1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

MOGADISHU : Mahasimu wa Somalia wajiandaa kwa vita

8 Novemba 2006
https://p.dw.com/p/CCuq

Wapiganaji wa Mahkama za Kiislam na wanamgambo wanaoiunga mkono serikali ya mpito nchini Somalia leo wamekuwa wanajiandaa kwa mapigano mapya kusini mwa nchi hiyo wakati maelfu ya watu wakikimbia mapambano hayo na mafuriko yaliosababisha maafa.

Muungano wa wanamgambo wanaoiunga mkono serikali wa Bonde la Juba wamesema wamejiandaa kujihami kutokana na vikosi vya Kiislam vinavyosogelea ngome yake kuu katika eneo la Gedo ambalo limeathirika vibaya na mafuriko makubwa wakati wa usiku kutokana na kufurika kwa kingo za mto.

Wakati hayo yakijiri kiongozi mwandamizi kabisa wa Baraza la Mahkama za Kiislam Sheikh Hassan Dahir Aweys amesema leo hii kwamba makubalano ya amani yanaweza kufikiwa kwa nchi yake ya Pembe ya Afrika lakini iwapo tu Ethiopia itaondowa wanajeshi wake walioko nchini Somalia hivi sasa wakiihami serikali ya mpito ya nchi hiyo.