1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

MOSCOW: Putin asema hakuna mzozo na Umoja wa Ulaya

16 Mei 2007
https://p.dw.com/p/CC1Y

Mawaziri wa nje wa Ujerumani na Marekani wamekuwa na mikutano mbali mbali pamoja na rais wa Urusi Vladimir Putin mjini Moscow.Baada ya kukutana na waziri wa nje wa Ujerumani,Frank-Walter Steinmeier,rais Putin alisema,hakuna mgogoro wo wote kati ya Umoja wa Ulaya na Urusi bali kuna tofauti za maoni tu juu ya njia za kutenzua masuala kadhaa.Kwa upande mwingine waziri wa nje wa Marekani Condoleezza Rice na Putin walikubaliana kuwa nchi zao zapaswa kuchukua hatua za kuboresha uhusiano kati ya nchi hizo mbili,ambao hivi sasa unajikuta katika hali ya mvutano.Lakini baada ya mkutano huo wa Moscow, waziri Rice alisema,Urusi haiwezi kutumia kura ya turufu kupinga mpango wa Marekani kutaka kuweka makombora ya ulinzi barani Ulaya.Urusi inapinga mradi wa ulinzi wa kujikinga dhidi ya makombora ambao Marekani inatazamia kujenga nchini Poland na Jamhuri ya Czech.Moscow vile vile inaukataa mpango wa Umoja wa Mataifa unaoungwa mkono na Marekani kuhusu Kosovo.Mpango huo unapendekeza kulipa jimbo la Serbia la Kosovo uhuru wa aina fulani chini ya usimamizi wa kimataifa.