1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

MOSCOW: Watu zaidi ya 150 wauwawa kwenye ajali ya moto

20 Machi 2007
https://p.dw.com/p/CCHF

Watu takriban 63 wameuwawa wakati moto ulipozuka katika nyumba ya wazee kusini mwa Urusi mapema leo. Wazima moto walihitaji zaidi ya saa nzima kuyafikia makazi hayo katika eneo la Krasnodar. Watu wengi walikufa kutokana na moshi mwingi.

Ajali hiyo ya moto ni ya hivi karibuni kutokea katika shule, mabweni, hospitali na tasisi za serikali ambazo zimeikumba Urusi katika miaka ya hivi karibuni.

Sambamba na taarifa hiyo, waokoaji nchini Siberia wanafanya jitihada za kuwaokoa wachimba migodi 13 ambao bado wamekwama ndani ya mgodi wa makaa ya mawe baada ya mripuko wa gesi ya methane kuwaua wafanyakazi zaidi ya 100 hapo jana.

Timu za uokozi zimefaulu kuwaokoa zaidi ya wanaume 90. Takriban wachimba migodi 200 walikuwa ndani ya mgodi huo wakati mripuko huo ulipotokea katika eneo la Kemerovo huko Siberia, yapata kilomita 3,500 kutoka mjini Moscow.

Uchunguzi unaendelea kutafuta kilichosababisha mripuko huo. Waziri mkuu Mikhail Fradkov ametoa mwito hatua madhubuti za usalama zichukuliwe baada ya ajali hiyo mbaya katika migodi ya Urusi katika kipindi cha zaidi ya muongo mmoja.