1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Moto mkubwa waendelea kuitafuna Marekani

Tuma Provian Dandi24 Oktoba 2007

Baada ya serikali ya Marekani kuokoa watu zaidi nusu milioni kutokana na moto mkubwa huko Calfornia na maeneo mengine, maelfu wengine wameambiwa kuondoka mara moja katika sehemu zinazoweza kufikiwa na moto huo

https://p.dw.com/p/C77Y
Gavana wa jimbo la Calfornia Anold Schwarzeneggar akishuhudia moto huo
Gavana wa jimbo la Calfornia Anold Schwarzeneggar akishuhudia moto huoPicha: AP

Baada ya kufanikiwa kuokoa wastani wa watu laki tano hadi sasa, serikali ya Marekani imewaagiza raia wake wanaoishi katika maeneo mengine yanayoweza kukumbwa na moto huo kuondoka mara moja.

Leo hii ikiwa ni siku ya nne tangu kutokea kwa moto mkubwa uliokwisha sababisha hasara kubwa katika jimbo la Calfornia na kwingineko, uzimaji wake umeendelea kuwa mgumu pamoja na serikali ya Marekani kupekelea askari wa kuzima moto wanaofika elfu kumi.

Kwa mujibu wa taarifa, zaidi ya nyumba elfu moja zimeshateketea kutokana na moto huo, pamoja na kuunguza eneo linalokadiriwa kufika kilometa za mraba elfu 1 na 220, huku ukisababisha kifo cha mtu mmoja.

Kusambaa zaidi kwa moto huo kunatokana na kasi ya upepo unaovuma kutokea maeneo ya Magharibi hivyo kuusambaza hadi sehemu ya kusini karibu na mpaka wa Mexico.

Rais George Bush amepanga kutembelea jimbo hilo la Calfornia hapo kesho baada ya kuutangaza moto huo kuwa janga la kitaifa miongoni mwa taifa saba.

Janga la moto huo linasemekana kuwa na athari kubwa kwa Wamarekani kama ilivyokuwa kwa janga la kimbunga aina ya Katrina kilichoitikisa nchi hiyo miaka miwili iliyopita, kwa kuathiri maisha ya watu na mali zao, pamoja na kuharibu miundombinu mingi.

Awali Gavana wa Jimbo la Calfornia Bwana Anold Schwarzenegger amesema kuwa moto huo umesababisha hasara ya mamilioni ya dola na utaathiri uchumi wa nchi kiasi kikubwa.

Bwana Schwarzenegger aliyekuwa kwenye eneo la tukio amesema hali hiyo inasikitisha na isiyoweza kusahaulika katika hisia za Wamarekani.

Wataalamu wa masuala ya hali ya hewa wanasema huenda moto huo unaweza kupunguza makali ikiwa kasi ya upepo katika maeneo ya Santa Anna itapungua, hali wanayoitegemea kutokea kuanzia sasa.

Wanasayansi hao wameongeza kwa kusema kwamba matumaini mengine yanaweza kutokea ikiwa maeneo ya kusini mwa jimbo la Calfornia lenye unyevunyevu mwingi yatapeleka mkondo wa unyevunyevu kwenye ukanda unaoungua.

Wakati jimbo la Calfornia likihaha kutokana na moto huo, wakazi wa San Diego pia wako katika harakati nyingine, kutokana na moto ulioyakumba maeneo manne na kusababisha maelfu ya raia kuyakimbia makazi yao.

Maeneo mengine yaliyokumbwa na moto huo unaosemekana kuwa mkubwa na wa kihistoria nchini Marekani ni Santa Barbara, Ventura, Los Angeles, Malibu, Ramona na Tijuana.