1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mshindi wa "Blogi Bora" atoka Tunisia

Abdu Said Mtullya21 Juni 2011

Mwanablogi maarufu kutoka Tunisia, Lina Ben Mhenni, ametunukiwa tunzo ya blogi bora kabisa kutokana na mchango wake katika kuwahamasisha watu juu ya masuala ya kijamii na kisiasa kupitia blogi yake ya "Tunisian Girl".

https://p.dw.com/p/11gIZ
Mshindi wa"Blogi Bora" Lina Ben Mhenni kutoka Tunisia.Picha: DW

Sherehe za kumkabidhi tuzo hiyo zimefanyika kwenye kongamano la Dunia la vyombo vya habari Deutschewelle Global Media lililoandaliwa na Deutschewelle mjini Bonn.

Tokea harakati za kuleta mapinduzi zianze katika nchi za kiarabu mitandao ya kijamii imekuwa hadithi ya kila mtu duniani. Na tokea wakati huo watu wanazungumzia juu ya mapinduzi ya Facebook. Watu wangeliweza kuyaleta mapinduzi kwa kujitokeza barabarani. Lakini mtandao wa internet umesaidia katika kuyaandaa mapinduzi hayo.

Mama huyo wa Tunisia alietunukiwa tuzo ya Blogi bora , Lina Ben Mhenni pia ametoa mchango wake kwa kutayarisha blogi inayoitwa " msichana wa Tunisia." Ni kutokana na mchango huo kwamba jana jioni mama huyo alitunukiwa tuzo ya blogi bora kwenye kongamano la dunia la vyombo vya habari lililoandaliwa na Deutschewelle linalofanyika mjini Bonn.

Mama huyo ambaye pia ni mhadhiri kwenye chuo kikuu cha Tunis ametunukiwa tuzo inayoitwa Blogi bora. Waamuzi 12 wa kimataifa waliichagua blogi ya mwanablogger huyo mnamo mwezi wa Aprili kuwa bora.

Mada ya mwanablogger huyo inahusu maendeleo ya kijamii na kisiasa nchini Tunisia lakini pia juu ya udhalimu na kubanwa kwa vyombo vya habari chini ya utawala wa Rais wa hapo awali nchini Tunisia Ben Ali aliepinduliwa kutokana na harakati za kimapinduzi za umma wa Tunisia.

Hata hivyo kazi ambayo mwanablogger huyo ameifanya haikuwa bila ya hatari. Amesema polisi wa Tunisia walitanda kila mahala na waliwaandama wanaharakati. Mwanablogger huyo ameeleza kuwa watu wengi walikamatwa na kuwekwa ndani. Wengine hata waliuawa. Lakini pamoja na mchango alioutoa, Lina Ben Mhenni amefadhaishwa na matukio ya hivi karibuni. Aliamua kuacha kazi aliyokuwa anaifanya kwenye kamati ya mashauriano ya kuleta mageuzi katika vyombo vya habari vya nchini Tunisia.

Amesema alichukua hatua hiyo kwa sababu hakuweza kuona mafanikio. Amejiuzulu kutoka kwenye kamati hiyo, kwa kuwa vyombo vya habari ni vilevile vilivyofanya kazi chini ya utawala wa Rais Ben Ali.

Katika kuamua juu ya Blogi bora safari hii mkazo uliwekwa katika mapinduzi yanayofanyika katika nchi za kiarabu na kaskazini mwa Afrika.

Tuzo ya Blogi bora imetolewa kwa mara ya saba mwaka huu na sasa imethibiti kuwa miongoni mwa nishani muhimu katika medani ya vyombo vya mawasiliano ya mtandao wa internet.

Mwandishi/Mathias von Hein/DW-intern/

Tafsiri/Mtullya Abdu/

Mhariri/Abdul-Rahman/