1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mshukiwa wa nne akamatwa kuhusiana na shambulio la Barcelona

John Juma
18 Agosti 2017

Kwa mujibu wa Maafisa wa polisi wa Uhispania, washukiwa waliokamatwa kuhusiana na mashambulizi ya Barcelona wametambuliwa kuwa ni raia watatu wa Morocco na mmoja ni raia wa Uhispania.

https://p.dw.com/p/2iTcQ
Spanien | Lieferwagen fährt in Barcelona  in eine Menschenmenge | Polizei und Forensiker untersuchen den Tatort
Picha: REUTERS/Stringer

Maafisa wa polisi nchini Uhispania wamesema kuwa bado hawajamtambua mshukiwa wa shambulizi la kigaidi aliyeliendesha gari na kuwagonga watu, ambapo kufikia sasa watu 14 wameripotiwa kuuawa na zaidi ya mia moja kujeruhiwa. Kufikia sasa, washukiwa wanne wamekamatwa na kutambuliwa. Na huko nchini Finland, polisi wamempiga risasi na kumkamata mwanaume anaeshukiwa kuwachoma visu watu kadhaa katika mji wa magharibi wa Turku.

Kwa mujibu wa Maafisa wa polisi wa Uhispania, washukiwa watatu waliokamatwa kuhusiana na mashambulizi ya Barcelona wametambuliwa kuwa ni raia wa Morocco na mmoja ni raia wa Uhispania.

Mpango wa mashambulio makubwa watibuka

Nyumba mjini Alcanar ambako mlipuko wa Jumatano ulitokea
Nyumba mjini Alcanar ambako mlipuko wa Jumatano ulitokeaPicha: picture-alliance/dpa/Europa Press/Bombers De La Generalitat

Josep Lluis Trapero ambaye ni afisa mkuu wa polisi wa Catalonia amesema mashambulizi hayo yalipangwa kwa muda mrefu na kuwa yalidhamiriwa kuwa misururu ya mashambulizi makubwa. Lakini mlipuko uliotokea katika nyumba moja siku ya Jumatano katika mji wa Alcanar ulivurunga mpango wa uhalifu huo kwani walikosa vifaa vya kutelezea mipango ya mashambulizi hayo makubwa.

Mlipuko huo wa Alcanar ulisababisha kifo cha mtu mmoja na ulitokana na jaribio la kutengeneza vilipuzi. Josep Trapero anaendelea kusema: "Kuhusiana na ukamataji, tumewakamata washukiwa 4. Mmoja alikamatwa Alcanar na alikuwa miongoni mwa waliojeruhiwa wakati wa mlipuko, na watatu wamekamatwa katika mji wa Ripoll. Hakuna yeyote kati yao anyechunguzwa kuhusiana na ugaidi kwa vile hakuna yeyote mwenye historia ya ugaidi."

Askari wanamtafuta ndugu yake mshukiwa mmoja wanayemzuilia ila hawajajua ikiwa huyo anayetafutwa ndiye dereva aliyeliendesha gari lililowagonga na kuwaua watu mjini Barcelona. Mshukiwa anayetafutwa ametambuliwa kuwa ni Moussa Oukabir, ambaye ni ndugu yake Driss Oukabir, raia wa Morocco ambaye alikamatwa jana na polisi katika mji wa Ripoll kilomita mia moja Kusini ya Barcelona.

​Watu wakusanyika Barcelona kuwaomboleza waliouawa
​Watu wakusanyika Barcelona kuwaomboleza waliouawaPicha: picture alliance/ZUMAPRESS.com

Uchunguzi zaidi

Uchunguzi unapoendelea, maafisa hao wa polisi wamesema kuwa wamemkamata mshukiwa mwengine, hivyo kufikisha idadi ya watu wanaoshikiliwa na polisi kuhusiana na mashambulio hayo kuwa wanne.

Polisi ilisema kuwa, afisa wao mmoja aliwapiga risasi washukiwa wengine watano na kuwaua katika eneo la Cambrils, Kusini mwa mji wa Barcelona baada ya watu hao kuliendesha gari dogo, na kuwagonga watu ambapo watu sita na afisa mmoja wa polisi walijeruhiwa. Kulitokea ufyatulianaji wa risasi na hapo ndipo afisa wa polisi akawaua washukiwa hao.

Raia mmoja aliyejeruhiwa kufuatia shambulizi la cambrils aliaga dunia na hivyo kufanya idadi ya waliofariki kutokana na mashambulizi ya Barcelona na Cambrils kufikia watu 14.

Shambulizi Finland

Picha hii iliyopigwa kwa kutumia simu ya mkononi inaonesha sehemu ya mji wa Turku ambako watu kadhaa walidungwa kisu Ijumaa
Picha hii iliyopigwa kwa kutumia simu ya mkononi inaonesha sehemu ya mji wa Turku ambako watu kadhaa walidungwa kisu IjumaaPicha: Getty Images/AFP

Na huko nchini Finland, maafisa wa polisi wamempiga risasi mguuni jamaa aliyeshukiwa kuwadunga watu kisu katika mji wa Turku. Mashirika ya habari nchini humo yameripoti kuwa watu 6 wamejeruhiwa miongoni mwao mwanamume mmoja na wanawake watano. Maafisa wa polisi wametoa tahadhari kwa watu kuepuka sehemu ya mji huo ambacho kisa hicho kimetokea.

Punde tu baada ya kuongozwa na Waziri Mkuu wa Uhispania Mariano Rajoy na Mfalme Felipe wa VI katika kuwaomboleza waliouawa kwa dakika moja ya kunyamaza kimya, watu waliokusanyika mjini Barcelona walisikika wakisema kwa sauti za juu, "not afraid, not afraid" kumaanisha hatuogopi, hatuogopi.

Mashambulizi hayo yamewaathiri rais kuwa nchi 34. Viongozi mbalimbali wa ulimwengu wametuma risala zao za rambirambu huku wakikemea mashambulizi hayo. Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Sigmer Gabriel na mwenzake wa Ufaransa wamesema wanaelekea Barcelona leo kuonesha umoja na ushirikiano wao na walioathiriwa.

Mwandishi: John Juma/DPEA/RTRE/AFPE

Mhariri: Iddi Ssessanga