1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jee nia imetoweka kuhusu hali ya Ugiriki?

30 Juni 2015

Mgogoro wa Ugiriki umeshaingia katika hatua mbaya sana ambapo bila ya msaada wa haraka nchi hiyo itafilisika. Katika maoni yake mwandishi wetu anautathmini msimamo wa Ujerumani juu ya mgogoro wa Ugiriki.

https://p.dw.com/p/1Fq1w
Zeitungen mit Schlagzeilen zum möglichen Grexit in Athen
Picha: imago/ZUMA Press

Jee Kansela wa Ujerumani ,Angela Merkel, mwanamke mwenye uzito mkubwa kabisa wa kisiasa barani Ulaya atakuwapo wapi katika wiki hii ya kuamua juu ya Ugiriki?

Ni wazi kwamba hatakuwamo katika kurasa za kwanza za magazeti ya nchini Ugiriki. Kansela Merkel ameweza kuepusha kuzingatiwa kama jahili, alievaa sare ya mafashisti, kama jinsi ilivyokuwa katika siku za nyuma.

Ishara ambazo Kansela wa Ujerumani anaziwasilisha ni za wazi kabisa: Ujerumani,na yeye, kama Mkuu wa serikali siyo wanaoamua juu ya neema ama madhila. Ujerumani ni nchi mojawapo miongoni mwa 28 za Umoja wa Ulaya na pia ni mojawapo miongoni mwa 19 za Ukanda wa sarafu ya Euro. Hakuna kiongozi anaeyapitisha maamuzi peke yake kwenye Umoja wa Ulaya,bali ni wote kwa pamoja.

Kansela Merkel mnamo wiki hii muhimu ameadhimisha mwaka wa 70 tangu kuundwa chama chake cha CDU. Na katika hotuba yake ya maadhimisho rasmi, bibi Merkel alisisitiza kwamba Bara la Ulaya linasonga mbele kutokana na uwezo wake wa kufikia mwakafa .

Mwandishi wa maoni Engel Dagmar
Mwandishi wa maoni Engel Dagmar

Maadili lazima yazingatiwe

Bibi Merkel pia amesisitiza juu ya kuzingatia taratibu zilizopo: za mshikamano na kuwajibika. Amesema ikiwa watu wa Ulaya watazikiuka taratibu hizo, watakuwa wanayasaliti maadili yao.

Angela Merkel amepongezwa na aliekuwa Kansela wa Ujerumani wa hapo awali Helmut Schmidt kwa uongozi wake makini katika juhudi za kuutatua mgogoro wa Ugiriki. Schmidt, aliekuwa Kansela kutoka chama cha Social Demokratik amesema anavutiwa na uongozi wa Bibi Merkel katika suala la Ugiriki.

Lakini katika wasaa huo ambapo Ujerumani inaongoza juhudi za kuutatua mgogoro wa Ugiriki, baadhi wanazikumbuka tena enzi za ufashisti; na kutokana na hayo, serikali nyingine za Ulaya zingelisimama dhidi ya Ujerumani .

Lakini sasa matarajio juu ya Ujerumani yamekuwa mengine. Duniani kote na katika vyombo vya habari, mtu wakati wote analikuta swali lile lile.Jee Angela Merkel yuko wapi? Rais wa Ujerumani, mawaziri wa ulinzi na wa mambo ya nje siku nyingi wamezungumzia juu ya Ujerumani kuuchukua wajibu mkubwa zaidi wa uongozi katika masuala ya kimataifa.

Ikiwa Euro itaanguka,Ulaya pia itaanguka

Na mwanzoni mwa wiki hii muhimu ,Kansela Angela Merkel ametoa kauli muhimu, Amesema ikiwa sarafu ya Euro itaanguka basi Ulaya pia itaanguka.
Lakini anapaswa kuitekeleza kauli hiyo kwa matendo.Anapaswa kusema mimi ndiye kiongozi wa nchi yenye nguvu kubwa za kiuchumi kuliko nyingine yoyote katika Umoja wa Ulaya ninayefanya kila juhudi ili bara la Ulaya lisianguke.

Mwandishi:Engel, Dagmar

Mfasiri:Mtullya Abdu.

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman