1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mugabe asema kamwe ardhi ya Zimbabwe haitachukuliwa tena na wazungu

Kalyango Siraj18 Aprili 2008

Mugabe ameishutumu Uingereza kwa kuchochea ghasia nchini mwake

https://p.dw.com/p/DkRW
Rais Robert Mugabe, katikati , akimkaribisha rais wa Afrika Kusini Thabo Mbeki, kushoto kwake, katika uwanja wa ndege wa,Jumamosi, April, 12, 2008.Picha: AP

Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe katika hotuba yake ya kwanza tangu kufanyike uchaguzi mkuu wiki tatu zilizopita,ameapa leo kuwa mkoloni wa zamani wa taifa hilo,Uingeraza pamoja na chama cha upinzani cha Movement for Democratic Change, MDC, kuwa kamwe 'hawataiba' nchi yake.

Rais wa Zimbabwe,akihutubia umati uliokusanyika katika uwanja wa michezo mjini Harare, wakati wa kuadhimisha miaka 28 ya uhuru wa nchi hiyo,amewapiga zii wa Ingereza na pia 'wezi' wanaotaka kuiba ardhi ya Zimbabwe.

Alizungumza kwa mda wa zaidi ya saa moja na mara kadhaa alikuwa akiiacha hotuba yake iliotayarishwa rasmi na kusema maneno ambayo huenda hayakuwa katika hotuba yake, ameishutumu Uingereza kwa kuchochea ghasia nchini mwake.

Wakati mmoja aliwauliza waliokuwa wanamsikilza ikiwa wangetaka Uingereza irejee tena kuwatawala?

Aliwaambia kuwa wao wenyewe walishuhudia Waingereza walichofanya waliposikia kuwa eti MDC ilikuwa inashinda.

Ameongeza kuwa wazungu wa Uingerza,Australia na Afrika Kusini wameanza kwenda Zimbabwe akiongeza kuwa baadhi yao baado wako katika mahoteli ya nchini humo.

Akasema kuwa jambo la kuwarejeshea wazungu ardhi ya Zimbabwe,kamwe halitafanyika.

Mugabe pia anasemekana amedai kuwa baadhi ya wazungu waliweka vizuizi vya barabarani katika njia zinazoelekea katika ardhi waliokuwa wanalimia na hivyo kuchokoza maveterani wa vita.

Makundi ya wanaoitwa maverani wa vita yamewafuikuza wazungu wengi kutoka katika mashamba yao na pia kuwafukuza wafanyakazi wao wa kiafrika.

Hotuba kali ya Mugabe imekuja siku moja tu kabla ya tume ya uchaguzi kuanza zoezi la kuhesabu upya baadhi ya kura zilizopigwa Machi 29 katika uchaguzi mkuu wa urais na bunge,ingawa matokeo ya urais baado kujulikana.

Kuhusu lawama dhidi ya Mugabe kuwa anakiuka haki za binadamu,hakuna utawala unaoheshimu sheria na kuwa hakuna demokrasia,Mugabe amesema leo kuwa demokrasia ililetwa tu nchini humo baada ya kuondoka kwa wakoloni.

Amesema kuwa wao ndio wameleta demokrasia ya mtu mmoja kura moja .Pia ndio wao walioleta demokrasia iliofuta ubaguzi wa rangi na wa jinsia na pia kuheshimu haki za binadamu.

Mugabe amesema pia kuwa wao ndio walimaliza dhulma zilizokuwepo nchini humo.

Na hayo yakiendelea katika nchi jirani ya Afrika Kusini kumetokea taarifa kuwa utawala wa Mugabe uliagiza silaha kutoka China.Silaha hizo sasa zimekwama katika bandari ya Durban kwa madai kuwa wafanyakazi huko wamegoma kupakua kutoka meli shehena hiyo na pia kuipakia na baadae kuisafirisha hadi Zimbabwe.

Chama cha cha Afrika Kusini kinachowaunganisha wachukuzi pamoja na wafanyakazi wengine nchini humo cha SATAMU, kinasema kuwa kinapanga maandamano katika bandari ya Durban kwani itakuwa si sawa kwa shehena hiyo kukubaliwa kwenda Zimbabwe ambako hali ya wasiwasi inazidi kutanda wakati ikisubiriwa matokeo ya uchaguzi mkuu wa urais uliofanyika wiki tatu zilizopita.

Meli ya China ilio na shehena hiyo miongoni mwa silaha zingine ni: risasi millioni tatu za bunduki za AK 47; mabomu ya roketi 1,500 pamoja na mizinga aina ya Mortar, baado imetia nanga katika bandari ya Durban.

Chama cha upinzani nchini Zimbabwe, cha Movement for Democratic Change ,MDC,kimelaumu chama cha Mugabe cha ZANU PF kwa kupanga kilichoita vita dhidi ya watu kufutia uchaguzi mkuu unaozusha utata wa mwezi jana.Upinzani unadai kuwa makundi ya mgambo yanaounga mkono Mugabe yanapewa silaha.