1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Musharraf kuondoa utawala wa hali ya hatari Desemba 16

30 Novemba 2007
https://p.dw.com/p/CUxD

Rais Pervez Musharraf wa Pakistan amesema kwamba anakusudia kuondowa utawala wa hali ya hatari nchini humo hapo tarehe 16 mwezi wa Desemba na kurudisha utawala wa katiba.

Ametangaza nia yake hiyo mjini Islamabad baada ya kuapishwa kwa kipindi kipya cha miaka mitano madarakani akiwa rais wa kiraia.Musharraf hapo Jumaatano amejiuzulu wadhifa wake wa mkuu wa majeshi akiwa chini ya shinikizo la kimataifa.

Wakati uchaguzi wa bunge ukiwa umepangwa kufanyika nchini humo hapo tarehe nane mwezi wa Januari Musharraf amevitaka vyama vyote vya kisiasa kushiriki uchaguzi huo ambapo mpinzani wake mmoja waziri mkuu wa zamani Benazir Bhutto amesema chama chake kitashiriki uchaguzi huo lakini kina haki ya kujitowa inapobidi kufanya hivyo.

Bhutto anasema wanashiriki uchaguzi huo katika hali ya kupinga kwamba hali ni ngumu dhidi ya upinzani lakini wanahisi iwapo watasusia uchaguzi huo hapo tena serikali itakuwa haina haja ya kuuhujumu uchaguzi huo na dunia itakuja kusema kwamba uchaguzi ulikuwa wa haki.

Hata hivyo wazir mkuu mwengine wa zamani Nawaz Sharif amesema muungano wake wa vyama vya upinzani utasusia uchaguzi huo.