1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mwanasheria mkuu wa Trump kukabiliwa na maswali kuhusu Urusi

Jane Nyingi
13 Juni 2017

Mwanasheria mkuu wa Marekani Jeff Sessions  leo atafika  mbele ya kamati ya ujasusi ya  baraza la Seneti, ambapo anatazamiwa kujibu maswali kuhusu uhusiano wake na Urusi.

https://p.dw.com/p/2ecBy
USA Jeff Sessions Rede in St. Louis
Picha: Reuters/L. Bryant

Swala lingine ni  kutoa majibu kuhusu jukumu lake  katika kutimuliwa aliyekuwa mkurungezi  wa Shirika la Upelelezi la Marekani – FBI, James Comey. Hii itakuwa mara ya kwanza  kwa mwanasheria huyo mkuu  kutoa ushahidi mbele ya umma  tangu  kuteuliwa na rais Donald Trump na  kuidhinishwa  mwezi Februari mwaka huu. Kikao hicho kinafanyika wakati mivutano ya  kisiasa ikiendelea katika mji mkuu wa Marekani Washington,kufuatia  ushahidi  wa Comey mbele ya kamati hiyo  wiki iliyopita uliozungukwa na hisia kali,huku nae rais Trump  akieleza kutoridhishwa na Sessions,mmoja wa watu walioshiriki pakubwa katika kampeini yake ya kuchaguliwa kuwa rais.

Utata kuhusu kutimuliwa Comey

Katika kikao hicho  Alhamisi iliopita  Comey alisema shirika la upelelezi  la Marekani-FBI lilifahamu taarifa ambazo zingetatiza Sessions kushiriki katika uchunguzi wa madai ya Urusi kuingilia uchaguzi mkuu wa Marekani mwaka uliopita. Comey alisema  atatoa maelezo zaidi katika  mazingira ya faragha,na hivyo kuzua wasiwasi  kuhusu  kitakochoulizwa na majibu ya kikao cha leoRais Trump alimtimua kazi Comey mapema mwezi uliopita. Huku ikizingatiwa alikuwa akisimamia  uchunguzi kuhusu kuwepo uwezekano wa uhusiano kati ya timu ya kampeni ya Trump na serikali ya Urusi.  Kutimuliwa kwa kwake kulizua maswali kuhusu sheria kuekewa vipingamizi.Lakini Sessions ambae alipendekeza  kutimuliwa Comey,huenda  akatumia cheo chake kuepuka kueleza mengi mbele ya kamati hiyo ya  seneti

USA Anhörung James Comey, früherer FBI-Direktor
James Comey alipofika mbele ya kamati ya ujasusi ya baraza la SenetiPicha: Getty Images/AFP/S. Loeb

Amri ya Trump yapuuzwa

Wakati hayo yakijiri , Mahakama nyengine  ya rufaa imelipinga   agizo la rais Donald Trump la kuwapiga marufuku  watu kutoka mataifa sita ya kiislamu kuingia marekani.Mataifa hayo  ni Iran,Libya,Somalia,Sudan,Syria na Yemen.Jopo la majaji watatu lilisema amri hiyo inakiuka  sheria zilizopo za kuhusu uhamiaji .Hata hivyo mahakama hiyo  mjini San Fransisco haikusema iwapo serikali inahitajika kuzipitia upya taratibu za ukaguzi kwa watu wanaoingia nchini humo. Rais Trump amekuwa akikabiliwa na upinzani mkali kwa  baadhi ya maamuzi  yake ambayo amekuwa akiyafanya tangu kuingia madarakani.

Mwandishi:Jane Nyingi AP/AFP
Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman