1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mzozo wa Gaza-Mashirika ya misaada yajiondoa.

Eric Kalume Ponda8 Januari 2009

Mashirika ya kutoa misaada ya kibinadamu katika eneo la Gaza yasimamisha mara moja shughuli zao kwa kutokana na kuendelea kuzorota kwa usalama katika eneo hilo na kuhofia usalama wao.

https://p.dw.com/p/GUfM
Wanajeshi wa Israel katika eneo la Gaza.Picha: picture-alliance/ dpa

Wanajeshi wa Israel waliendelea na mashambulizi yake kulenga vituo vya mpakani vinavyoshukiwa kutumiwa na wafuasi wa Hamas kuingiza silaha kwa njia ya magendo katika eneo hilo.


Wanajeshi wa Israel wameripotiwa walifanya mashambulizi makali karibu na mji wa mpakani wa Rafah kwenye mpaka Gaza huku kukitawanya vijikaratasi kuwaonya wakaazi wa eneo hilo kuhama.


Mashambulizi hayo yakiendelea wanajeshi zaidi wa vikosi vya umoja wa mataifa vilivyopelekwa nchini Lebanon kudumisha amani wamepelekwa kwenye mpaka wa Israel na Lebanon kufuatia shambulizi la mizinga lililotelekezwa mapema leo. Hata hivyo hakuna ripoti yoyote iliyotolewa kuhusu mashambulizi mapya katika eneo hilo.


Hali ilivyo katika eneo la mashariki ya kati inaweza kufananishwa tu na mchezo wa sinema.


Ndege za kivita za Israel zilifanya mashambulizi makali katika mji huo wa Rafah baada ya kutangaza kwamba litasimamisha mashambulizi kwa muda wa masaa matatu kila siku.


Walioshuhudia wanasema kuwa mashambulizi hayo pia yametekelezwa katika eneo la kusini mwa Gaza ambako watu 3 walijeruhiwa wakati jeshi hilo la Israel lilipoushambulia msikiti mmoja karibu na mji wa Gaza.


Hali kadhalika mashirika ya kutoa misaada yalisimamisha shughuli zao katika eneo hilo kufuatia kuendelea kuzorota kwa hali ya usalama na kuhofia usalama wao.


Hatua hii imechukuliwa baaeda ya mtu mmoja kuawa wakati wanajeshi wa Israel waliposhambulia msafara wa magari yaliyokuwa yakienda kusafirisha misaada ya kibinadamu katika eneo la kaskazini mwa Gaza.


Afisa wa huduma za kibinadamu wa umoja wa mataifa katika eneo hilo Chris Gunness, alisema kuwa msafara huo ulishambulia ulipokuwa ukielekea mji wa Erez.


Shirika la msalaba mwekundu limelishtumu vikali jeshi la Israel kwa kukiuka mkataba wa kimataifa kwa kushindwa kuwasaidia majeruhu katika vita hivyo. Shirika hilo linasema kuwa walipata watoto wanne waliodhofika wakililia maiti ya mama yao katika eneo hilo la mashambulizi.


Mashirika hayo yanasema kuwa hali inaendelea kuwa mbaya katika eneo hilo la Gaza, huku misaada ya kibinadamu iliyoweza kusafirishwa hapo jana hadi ndani ya eneo hilo ikitarajiwa kuwahudumia watu 2000 kwa muda wa wiki moja.


Zaidi ya watu 250 wa kigeni ambao wamekwama katika eneo hilo tangu mashambulizi hayo yaanze mwezi uliopita walishindikizwa kwa misafara ya shirika la msalaba mwekundu hadi hadi eneo la mpakani na Israel.


Hali kadhalika yaripotiwa kuwa wafuasi wa Hamas walijibu mashambulizi ya Israel kwa kurusha mizinga 4 ya roketi na kuwajeruhi raia watatu wa Israel karibu na mji wa mpakani wa Ein Hashlosha Kibbutz ulioko umbali wa kilomita 5 kutoka mpakani.


Mashambulizi hayo yanayoingia siku yake ya 13 hii leo yamesababisha watu 700 kuuawa na wengine zaidi ya 3,000 kujeruhiwa.


Afisa mmoja wa ngazi za juu wa Hamas Mohammed Nazzal ametoa taarifa kuwa Hamas itaendelea na mashambulizi yake dhidi ya Israel hadi pale Israel itaka sitisha mapigano na kuondoka katika ardhi yake.

Lakini rais wa Israel Shimon Peres anasema kuwa serikali yake inatambua juhudi zinazofanywa na jamii ya kimataifa kukomesha mapigano hayo lakini inawajibu wa kuwalinda raia wake. Rais Shimon Peres alisema ``Sisi tuliondoka Gaza kabisa, hawawezi kusema kuwa bado tunakalia eneo hilo kimabavu. Tunapasa kushauriana lakini hao Wapalestina hawataki mashauriano na Mtu yoyote. Tumefanya mashauriano na Abu Masna na hata Abbas´´.


Wakati hayo yakijiri, wanajeshi zaidi wamepelekwa kwenye eneo la mpakani baina ya Israel na Lebano katika juhudi za kuzuia kuendelea kwa mashambulizi zaidi kama yale yaliyoshuhudiwa mapema leo.


Msemaji wa vikosi hivyo Yasmin Bouziane alisema kuwa zaidi ya wanajeshi 13,000 wa vikosi vya umoja wa mataifa UNIFIL wameimarisha usalama katika eneo hilo kudumisha mkataba wa kusitisha mapigano uliofikiwa mwaka wa 2006 kati ya wapiganaji wa kundi la Hezbolla na Israel.


Mbunge mmoja wa Israel Ben Eliezer alisema kuwa shambulizi hilo lilitarajiwa kwani Lebanon limewahifadhi wafuasi wengi wa Hamas.


Kunahabari kuwa kuna zaidi ya wakimbizi 400,000 kutoka Gaza waliotorokea Lebanon ambao sasa wamekusanyika katika kambi 12 za wakimbizi nchini humo.


Habazi zaidi zinasema kuwa maelfu ya waandamanaji waliandamana katika barabara za miji ya Syria kushtumu vikali mataifa ya kiarabu wnayoyataja kuwa wasaliti.