1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mzozo wa madeni Ulaya

10 Novemba 2011

Rais wa baraza la Ulaya, Jose Manuel Barroso ametoa onyo kali kuhusu hatari iliyopo ya kuligawanya eneo linaloitumia sarafu ya euro wakati mzozo wa madeni unapozidi kuongezeka

https://p.dw.com/p/1385K
Jitihada za kuiokoa sarafu ya euroPicha: dapd

Rais wa baraza la Ulaya, Manuel Barroso amesema kuwa Ulaya inaweza kuimarika iwapo mataifa yote wanachama yatashirikiana. Aliongeza pia, kuwa mwanachama wa eneo linaloitumia sarafu ya euro, kunapswa kuufafanuwa Umoja wa Ulaya.

Projekt Connecting Europe Jose Manuel Barroso
Rais wa baraza la Ulaya Jose Manuel BarrosoPicha: dapd

Matamshi yake yamejiri baada ya Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel, na rais wa Ufaransa, Nicolas Sarkozy, kuitisha mageuzi makubwa ya kimuundo. Sarkozy alishinikiza kuwepo Ulaya iliyogawanyika kutokana na kasi ya ukuwaji wa mataifa, huku naye Merkel amesema kuwa ulimwengu hauwezi kusubiri Ulaya ijitatulie matatizo yake.

Wakati huo huo, Uchumi nchini Italia unazidi kudidimia. Rais wa nchi hiyo Giorgio Napolitano amejaribu kuyahakikishia masoko kwa kuahidi kuwa mpango wa mageuzi muhimu ya kiuchumi yatapitishwa bungeni kufikia Jumapili.

Waziri mkuu Silvio Berlusconi ameahidi kujiuzulu baada ya kupitishwa mageuzi hayo na aliyekuwa kamishna wa Umoja wa Ulaya Mario Monti amesifiwa kuwa huenda ndiye atakayemrithi Berlusconi. Viwango vya ukopeshaji Italia hapo jana vilipanda kwa zaidi ya asilimia 7, ikiwa ni kiwango kilicho isababisha Ugiriki, Ireland na Ureno kutafuta mikopo ya kimataifa.

Silvio Berlusconi
Waziri mkuu anayeondoka Italia Silvio BerlusconiPicha: dapd

Italia ni nchi ya pili iliyo na madeni makubwa katika eneo linaloitumia sarafu ya euro baada ya Ugiriki. Wachambuzi wengi wanaamini kuwa ni jitihada ya pamoja ya Umoja wa Ulaya, shirika la fedha la kiamataifa IMF na benki kuu ya Ulaya ndiyo inayoweza kuikoa nchi hiyo, na hivyo pia kuliokoa eneo zima linaloitumia sarafu hiyo ya euro.

Nchini Ugiriki, Waziri mkuu anayeondoka, George Papandreou, amelihotubia taifa kupitia televisheni akisema kuwa makubaliano yamefikiwa kuhusu kuunda serikali mpya ya mpito nchini humo.

Krise in Griechenland George Papandreou
Waziri mkuu anayeondoka Ugiriki George PapandreouPicha: dapd

Hatahivyo makubaliano hayo yalionekana kusambaratika baada ya chama kidogo kuondoka kwenye mazungumzo hayo jana jioni, huku kukiwepo maswali kuhusu ni nani atakayemrithi Papandreou. Majadiliano yanaendelea hii leo.

Serikali ya mpito inatarajiwa kuwa na jukumu la kutayarisha uchaguzi mwezi Februari na kutekeleza mageuzi kama inavyotakiwa na Umoja wa Ulaya na shirika la fedha la kimataifa, IMF, ili nchi hiyo iliyo na madeni iweze kupokea mikopo.

Mwandishi: Maryam Abdalla/Rtrs, AP, AFP