1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mzozo wanukia kati ya China na Marekani kuhusu ulinzi wa anga

Admin.WagnerD27 Novemba 2013

Ndege mbili za kijeshi za Marekani zimepita katika anga za China katika eneo linalozozaniwa kati ya China na Japan la visiwani bila ya kuiarifu na kupuuza agizo la China kutaka kuarifiwa mapema kutumika kwa anga zake.

https://p.dw.com/p/1APJN
Picha: Getty Images

Wataalamu wa masuala ya kidiplomasia wanaona ukiukaji huo wa masharti ya China kuhusu kutumika kwa anga zake kutoka kwa Japan na washirika wake Marekani kutachochea hata zaidi mzozo ulioko wa kusimamia eneo la visiwa kati ya Beijing na Tokyo na kuifanya China kuchukua hata hatua zaidi kusisitiza ubabe wake.

Mwishoni mwa wiki iliyopita China ilichapisha kanuni mpya za kuanzisha eneo maalum la ulinzi wa anga katika eneo lenye mzozo wa maji katika bahari ya China Mashariki na kutangaza kuwa ndege zinazopita katika eneo hilo la bahari, sharti zitii maagizo yake.

Ndege zitakazokuwa zikiingia katika eneo hilo zitatakiwa kutoa taarifa za awali kabla ya kupita katika eneo hilo na kudumisha mawasiliano kwa kujibu maswali yatakayohitajika kutoka kwa waongozaji ndege.

Chanzo cha mzozo ni visiwa

Eneo hilo la ulinzi linahusisha visiwa vya Senkaku na Diaoyu ambavyo vimekuwa chachu ya kuongezeka kwa mzozo baina ya mataifa hayo mawili. China imesema itadhibiti anga na visiwa vyake mashariki mwa nchi hiyo na kuonya kuwa itachukua hatua za dharura za kujilinda dhidi ya ndege yoyote itakayofeli kuzingatia sheria zake.

Chombo cha majini cha Kijeshi cha China kikishika doria
Chombo cha majini cha Kijeshi cha China kikishika doriaPicha: picture-alliance/AP

Profesa Sun Zhe wa chuo kikuu cha Tsinghua mjini Beijing amesema iwapo Marekani itaendesha ndege zake mara mbili tatu kama ilivyofanya wakati huu, basi itailazimu China kuchukua hatua ambazo hazitakuwa za maneno matupu tu.

Wizara ya ulinzi ya China imesema ilifuatilia nyendo zote za ndege hizo za kijeshi za Marekani jana lakini msemaji wa wizara ya ulinzi ya Marekani amesema ndege hizo hazikufuatiliwa wala hazikupokea mawasiliano yoyote kutoka China.

Shirika la ndege la Japan, ANA, limesema kufuatia ombi kutoka kwa serikali yake, limesitisha kutoa taarifa zozote za mipango ya safari za ndege zake kwa maafisa wa China na haijashuhudia matatizo yoyote wakati ikipita katika kanda hiyo na kuongeza hakuna kitisho kwa usalama wa abiria wake.

Japan yajiimarisha kukabiliana na vitisho

Hatua hiyo ya China pia inaonekana kutoa fursa kwa waziri mkuu wa Japan, Shinzo Abe, kupata mashiko ya hoja yake ya kupewa nguvu zaidi za kuboresha jeshi lake ili kukabiliana na vitisho vyovyote kutoka nje.

Rais wa Marekani Barrack Obama na waziri mkuu wa Japan Shinzo Abe
Rais wa Marekani Barrack Obama na waziri mkuu wa Japan Shinzo AbePicha: Reuters

Japan leo imeunda baraza la kitaifa la usalama ambalo limeidhinishwa na bunge linalompa waziri mkuu mamlaka zaidi kuhusu masuala ya kiusalama na sera za kigeni na ulinzi hatua inayoonekana kutokana na mzozo huu uliozuliwa upya na China.

Marekani ambayo ina mamia ya ndege za kijeshi katika kanda hiyo imesema haina nia ya kuzingatia kanuni mpya zilizowekwa na China huku Japan ikizitaja hatari na zisizokubalika. Taiwan na Korea Kusini ambazo pia ni washirika wa Marekani katika kanda hiyo pia zimetupilia mbali masharti hayo ya China.

Hata Australia imejiingiza katika mzozo huo kwa kumuita balozi wa China nchini humo kuelezea wasiwasi wao kuhusu maagizo hayo ya kudhibiti anga yake.

Mwandishi:Caro Robi/Reuters/Ap

Mhariri: Josephat Charo