1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

NATO yakutana Poland

19 Februari 2009

Ajenda kuchangia vikosi zaidi kwa Afghanistan

https://p.dw.com/p/GxGw
NATOPicha: AP

Mawaziri wa ulinzi wa Shirika la NATO, wanakutana leo Krakow,Poland kuzingatia upya mkakati wao juu ya Afghanistan huku Marekani ikijiandaa kupeleka huko askari 17,000 zaidi kupambana na wataliban.

Waasi hao pamoja nao wapiganaji wa Al Qaeda na wafanyabiashara ya magendo ya madawa ya kulevya wakiwa na kambi yao mgongoni nchini Pakistan, wanatoa changamoto kali hivi sasa kwa shirika kubwa kabisa la kijeshi duniani (NATO) wakati likipigana kukamilisha mradi wake muhimu kabisa -ushindi dhidi ya wataliban.

Maafisa wa hadhi ya juu wa kijeshi na wajumbe wa kibalozi wa nchi hizo za NATO, karibuni hivi wamekuwa wakiranda randa huku na huko barani Ulaya wakiijiandaa kuudurusu upya mkakati wa shirika lao nchini Afghanistan.

Serikali ya Rais Barack Obama ya Marekani, itawatarajia washirika wake wa NATO kuchangia zaidi wanajeshi wao nchini Afghanistan kabla ya kufanyika uchaguzi hapo August-hii ni kwa muujibu wa waziri wa ulinzi wa Marekani Robert Gates alivyoarifu jana.

"Serikali ya Marekani itayari ............kuchangia askari zaidi nchini Afghanistan ,lakini wazi itatarajia pia mchango kutoka kwa washirika wake "-alisema Gates.

Gates alisema hasa Marekani itawashikilia washirika wake kuongeza vikosi vyao hata ikiwa kwa kipindi kifupi kuelekea uchaguzi huo wa rais August 20. Hivi sasa kuna kiasi cha askari 70,000 wa kigeni nchini Afghanistan kati yao 38,000 ni wamarekani.

Katika kikao cha leo mjini Krakow,waziri wa ulinzi wa Marekani anatarajiwa kwahivyo, kuwashinikiza wenzake kuchochea kuni kupambana na wataliban.Sehemu kubwa ya wanajeshi 17.000 zaidi inaopeleka huko Marekani, watazamiwa kuwekwa kusini mwa Afghanistan ambako watalibanani wanatoa changamoto kali pamoja na kustawi huko kwa mavuno ya mimea inayotengezwa madawa ya kilevya kama opium.

Ukosefu wa wanajeshi na zana za kutosha kunapalilia mivutano miongoni mwa washirika wa NATO huku baadhi yao hawako tayari kupeleka askari wao kusini mwa Afghanistan wakati wale wa Marekani,Uingereza ,Kanada,Denmark na wale wa Holland wamekuwa wakiuwawa au kujeruhiwa.

Kamanda wa vikosi vya Marekani nchini Afghanistan, ameomba kikosi kingine kitakacho beba jukumu la kuvifunza vikosi vya ulinzi vya Afghanistan.

Mshirika mwengine wa NATO -waziri wa ulinzi wa Australia , ameonya leo kuwa hatazamii ushindi dhidi ya wapiganaji watalibani karibuni huko Afghanistan na kwamba Australia, haitachangia askari zaidi isipokuwa wanachama wa NATO wamejitolea nao kufanya hivyo.

Hatahivyo, askari 1000 wa Australia wanatazamiwa kusalia Afghanistan.Waziri huyo wa ulinzi Fitzgibbon, akizungumza huko Poland kabla ya kikao cha leo cha NATO .

Katibui mkuu wa NATO Jaap de Hoop Dcheffer amesema kuwa kiasi cha askari 10.000 watahitajiwa kusimamia usalama wakati wa Uchaguzi wa August 20.Lakini, alisema, ni wanachama wachache waliojitolea kuchangia askari zaidi.

Uchaguzi wa August nchini Afghanistan, unatazamiwa kutoa changamoto kali kwa juhudi za shirika la ulinzi la NATO za kueneza demokrasia katika nchi hii iliovurugwa kwa vita na mfarakano.