1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Nchi za Kiarabu za Ghuba na Diplomasia ya Marekani kuelekea Iran

Miraji Othman18 Februari 2009

Kujongeleana Marekani na Iran kunazitia wasiwasi nchi za Kiarabu

https://p.dw.com/p/GwoR
Rais wa Marekani, Barack Obama, akihojiwa na televisheni ya Kiarabu, al-ArabiyaPicha: AP

Nchi za Kiarabu katika Ghuba zinaanza kuwa na wasiwasi kwamba mkaribiano wowote wa Marekani na Iran unaweza mwishowe ukapelekea kuweko shida upande wao. Shida hiyo ni kuwa na nchi jirani isiokuwa ya Kiarabu ya madhehebu ya Kiislamu ya Shia ilio na silaha za kinyukliya. Nchi za Kiarabu katika Guba zilizo za madhehebu ya Kiislamu ya Sunni zilikuwa hazijavutiwa sana na msimamo mkali wa Rais wa zamani George Bush juu ya Iran, zikihofu kwamba uhasama wa nchi mbili hizo unaweza ukatapakaa katika eneo hilo lote...

Lakini nchi hizo za Kiarabu pia zina wasiwasi juu ya uwezekano wa kuboreka maingiliano baina ya Marekani na Iran, jambo ambalo limeashiriwa na rais Barack Obama, na kwamba rais huyo wa Marekani huenda akaenda umbali wa kuregeza kamba kwa Iran ilio na nguvu katika eneo la Ghuba. Nchi za Kiarabu kwa muda mrefu zimeiangalia Iran kwa jicho la wasiwasi na hata uhasama. Mustafa Alani wa Kituo cha Utafiti wa matoeko katika Guba kilio na makao yake Dubai, anasema Waarabu hawayapingi mashauriano yanayoendelea baina ya Marekani na Iran. Kinyume na hivyo, nchi hizo za Kiarabu zinatia moyo kuweko mdahalo wa aina hiyo. Hata hivyo, alisema mtaalamu huyo, Waarabu wana wasiwasi mkubwa kwamba Wamarekani huenda wakaregeza kamba kwa Wa-Irani kwa kiwango ambacho kinaweza kuhatarisha usalama wa nchi za Kiarabu, kitu ambacho hawatakikubali.

Rais Barack Obama alishinda uchaguzi wa urais wa Marekani kwa kuahidi kuleta mabadiliko, na akamteuwa mwakilishi wa amani katika Mashariki ya Kati katika wiki ya mwanzo baada ya kuingia madarakani. Pia alisema yeye yuko tayari kuwa na mdahalo na Iran katika juhudi za hadharani za kuwanyoshea mkono wa amani Waislamu. Bwana Alani alisema matakwa yao ya kimsingi ni kwamba Marekani isiregeze kamba juu ya mpango wa kinyukliya wa Iran na kujiingiza nhi hiyo katika Iraq, Lebanon na Palastina. Alisema nchi za Kiarabu hazitaki kushtushwa tu, zinataka kuwa mshirika na maslahi yao yanahitaji yawakilishwe.

Nchi za Kiarabu katika Guba, ambazo zilionya dhidi ya uvamizi wa Marekani katika Iraq hapo mwaka 2003, sasa zina hofu kwamba kuondoka mapema majeshi ya Kimarekani kutoka nchi hiyo, kama ilivoahidiwa na Barack Obama, kutaiwachia nchi hiyo katika mikono ya wanasiasa wa Kishia walio washirika wa Iran na ambao wemedhibiti madaraka baada ya kuondoshwa madarakani Saadam Hussein. Nchi hizo za Kiarabu zina hofu kwamba serekali ya Marekani ambayo haitataka kuchukuwa hatua za kijeshi dhidi ya Iran itashindwa kuzizuwia tamaa za Iran za kutaka kuwa na mpango wake wa kinyukliya, na mwishowe kuwabakisha Waarabu wa madhehebu ya Sunni wakibanwa baina ya madola mawili ya kinyukliya- Iran na Israel.

Lakini nchi hizo za Kiarabu za Ghuba zinatafautiana juu ya namna ya kukabiliana na mtihani huu. Mgawanyiko ulionekana wakati wa wiki tatu za mashambulio ya Israel huko Ukanda wa Gaza ambayo yaliwauwa zaidi ya watu 1,300 na kuziweka Saudi Arabia, Misri na washirika wao upande mmoja na Qatar, Iran, Syria na washirika wao upande mwengine.

Wachunguzi wa mambo wanasema maendeleo katika mwenendo wa amani baina ya Waarabu na Israel yatasaidia kuyapunguza makali ya Wa-Irani ambao washirika wao huko Libanon na Gaza wamechomoza katika vita vya karibuni wakionewa huruma zaidi kutoka kwa Waarabu na Waislamu wa kawaida. Hasa, pindi kutapatikana muwafaka wa amani baina ya Israel na Israel, basi jambo hilo linaweza likawaondoa Wa-Syria kutoka kambi ya Wa-Irani na kuitenga nchi hiyo. Na uamuzi wa Barack Obama kumtuma kwa haraka mwakilishi wake hadi Mashariki ya Kati umekaribishwa, japokuwa inagojewa kuonekana kama ataweza kuisukuma Israel na Wapalastina waliogawanyika katika meza ya mashauriano.

Lakini haifikiriwi kwamba Barack Obama kuzungumza moja kwa moja na Wa-Irani kutabadilisha malengo ya kimbinu ya marekani. Marekani haiko tayari mara moja kuukubali ubwana wa Iran katika eneo la Ghuba au nchi hiyo kuwa na silaha za kinyukliya.


Miraji Othman/Reuters