1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

NEW-YORK:Baraza la usalama laidhinisha vikosi kwenda Chad na Afrika ya kati

26 Septemba 2007
https://p.dw.com/p/CBMY

Baraza la usalama la Umoja wa mataifa limeidhinisha kwa pamoja kupeleka kikosi cha Umoja wa Ulaya na maafisa wa polisi wa Umoja wa mataifa katika nchi za Chad na jamhuri ya Afrika ya Kati kwa lengo la kuwalinda raia dhidi ya machafuko yanayotokana na mgogoro wa Jimbo la Darfur nchini Sudan.

Mawaziri wa Ulinzi wa Umoja wa Ulaya wiki iliyopita waliidhinisha hatua ya kutuma kikosi cha wanajeshi zaidi ya 4000 katika maeneo hayo wengi wakiwa kutoka Ufaransa kufikia mwishoni mwa mwaka huu.

Umoja wa mataifa umesema utatoa hadi askari 350 na maafisa wa kijeshi watakaohusika na shughuli za mawasiliano.

Rais Bush hapo jana akizungumzia juu ya maamuzi yaliyofikiwa na baraza hilo la usalama la Umoja wa mataifa kuhusu mgogoro wa Sudan,Chad na Jamhuri ya Afrika ya Kati alisema.

Tunataka maneno ya baraza hili kuwa na maana.Tunataka baraza linapowatetea watu wanaoteseka maneno yake yafuatwe na vitendo.

Umoja wa mataifa unakadiria kuna kiasi cha wakimbizi laki sita nchini Chad na jamhuri ya Afrika ya kati.Chad imesifu hatua ya kutumwa wanajeshi wa Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika pamoja na maafisa wa polisi katika jimbo la Darfur nchini Sudan.