1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ni wakati wa kuomboleza kifo cha 'tiki-taka'?

22 Mei 2014

Baada ya kushinda mataji matatu ya mashindano yaliyopita ya kimataifa, ni muhimu kuwaza kama mabingwa watetezi Uhispania huenda wakaambulia patupu katika dimba la Kombe la Dunia nchini Brazil

https://p.dw.com/p/1C4Nf
Bildergalerie Stars der EM 2012
Picha: picture-alliance/dpa

Msururu wa ajabu wa mafanikio bila shaka hatimaye utafikia kikomo, na kuna wasiwasi kuwa mfumo wao wa mchezo – unaoonyeshwa bayana na kiungo anayezeeka Xavi Hernandez – tayari umepitwa na wakati. Uhispania iliufuata mchezo wa Barcelona na kushinda Kombe la Dunia mwaka wa 2010 na Euro mwaka wa 2012. Katika Kombe la Dunia nchini Afrika Kusini, walipata ushindi mnono kwa kuwasambaratisha Italia magoli manne kwa sifuri kwenye fainali, lakini mbinu ambayo waliitumia kumiliki mecho za awali iliwafanya wengi kukitaja kikosi cha kocha Vicente del Bosque kukosa mvuto na yenye kuchosha.

Hata kama mchezo huo haukuvutia na kusisimua, ulikuwa na ufanisi. Lakini miaka miwili baadaye, iliyokuwa himaya ya Pep Guardiola katika klabu ya Barcelona imeporomoka.

Mfumo wa Catalans, wa kuumiliki mpira, unaofahamika kama ‘tiki-taka’, ulionekana kuwa dhaifu baada ya kufumuliwa na Bayern Munich, kutika safu zote kutoka ulinzi hadi ushambulizi, katika nusu fainali ya Champions League mwaka wa 2013.

Pep Guardiola hakuamini kichapo walichopewa na Real Madrid katika Champions League
Kocha wa Bayern Pep Guardiola hakuamini kichapo walichopewa na Real Madrid katika Champions LeaguePicha: Getty Images

Kisha mwaka mmoja baadaye, nao Bayern, chini ya uongozi wa Guardiola, walikuwa wakicheza ‘tiki-taka’ na kuraruliwa kupitia mashambulizi makali ya Real Madrid katika nusu fainali ya dimba hilo la Ulaya. Hivi karibuni, matokeo yake, imekuwa maarufu kwa kuomboleza kifo cha mfumo huo.

Mbinu mbadala za kucheza zimeibuka katika kiwango cha vilabu. Mchezo wa mashambulizi ya kasi wa Borussia Dortmund uliwafikisha katika fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya mwaka wa 2013, wakati Atletico Madrid wamepata mafanikio makubwa kwa kuutumia mfumo wa 4-4-2 unaotegemea safu imara ya ulinzi, idara ya kiungo na ushambuliaji wa kasi wa Diego Costa.

Jose Mourinho ameyapeleka mambo katika kiwango kikubwa kabisa wakati mwingine. Mbinu yake ni kuwa usipoutawala mpira utafany makosa machache na hivyo utaushinda mchezo.

Lakini kusema ‘tiki-taka’ imekufa ni kurukia tu maamuzi ya haraka. Baada ya yote, hadi kufikia mwaka wa 2011, Barcelona iliyoongozwa na Guardiola ilichanganya mfumo wao wa pasi fupi na mbinu moja muhimu, mchezo wenye nguvu wa kulishambulia lango la adui. Na Bayern yake Guardiola ikashinda mataji mawili nchini Ujerumani katika msimu uliomalizika.

Kocha wa Chelsea Jose Mourinho anafahamika sana kwa mbinu ya 'kuegesha basi' katika lango lao
Kocha wa Chelsea Jose Mourinho anafahamika sana kwa mbinu ya 'kuegesha basi' katika lango laoPicha: Getty Images

‘Tiki-taka’ inaweza bado kufaulu kama itachezwa na kasi inayostahiki, na Uhispania inatarajiwa kuweka imani katika mfumo huo ambao umewatendea mema katika mashindano ya awali.

Hata hivyo kuna mbinu nyigni za kushinda mechi, na zote ni halali. Kucheza na washambuliaji wawili, hakujatumika sana katika mwongo mmoja uliopita, na mifumo ya 4-2-3-1 na ule wa Barcelona wa 4-3-3 na mshambuliaji mmoja utakuwa maarufu sana nchini Brazil.

Lakini, timu kadhaa za America ya kati na Kusini zitacheza na washambuliaji wawili, ikiwa ni pamoja na Uruguay itakayowatumia Edinson Cavani na Luis Suarez, na Chile. Beki ya ulinzi ya wachezaji wanne itasalia kutumiwa, hata kama Mexico itapendelea safu ya ulinzi ya wachezaji watano naye Louis van Gaal amekiri kuwa kutokuwepo kwa kiungo wake Kevin Strootman kutokana na jeraha huenda kukaifanya Uholanzi kuwachana na mfumo wao wa 4-3-3 na kuzingatia ule wa 5-3-2.

Shirikisho la FIFA, lilisema katika Kombe la Dunia la mwaka wa 2010 nchini Afrika Kusini kuwa “mechi za ufunguzi za awamu ya makundi zilichezwa kwa tahadhari”. Mambo yaliimarika, lakini idadi ya wastani ya magoli katika kila mechi kwa kinyang’anyiro hicho ilikuwa 2.27, kiwango ambacho ni cha chini kabisa kuwahi kushuhudiwa, isipokuwa kile cha dimba la Italia mwaka wa 1999 (2.21). Uhispania ndio washindi waliofunga magoli machache kabisa tangu Kombe la Dunia lilipoanzishwa.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP
Mhariri: Hamidou Oummilkheir