1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Nigeria yafuata mkondo wa Afrika kusini yazabwa 2:1 na Ugiriki

17 Juni 2010

Argeina imeingia duru ijayo kwa kuichapa Korea Kusini 4:1

https://p.dw.com/p/NtwY
Kocha wa Ugiriki,mjerumani Otto Rehagel apongeza timu yake.Picha: AP

Nigeria, imefuata leo mkondo wa Bafana Bafana kuwa timu ya pili ya Afrika ilio hatarini kuaga Kombe la dunia 2010 duru ya kwanza baada ya kuzabwa mabao 2:1 na Ugiriki.

Kalu Uche, aliipatia Nigeria bao la kwanza kwa mkwaju wa Free-kick dakika ya 16 ya mchezo.Ugiriki ikiongozwa na kocha mjerumani.Otto Rehagel, alieitawaza mabingwa wa Ulaya,ilisawazisha mnamo dakika ya 43 ya mchezo,muda mfupi kabla mapumziko.Ugiriki,ilikua lazima ishinde ili kusalia katika kombe la dunia wakati Nigeria, ina nafasi hadi mpambano ujao na Korea ya Kusini,iliozabwa mabao 4:1 hivi punde na Argentina kujua hatima yake ya mwisho.

Je, kocha Otto Rehagel, baada ya kuwakuta wanigeria wanacheza na wachezaji 10 tu uwanjani, akageuza mbinu kuwanasa Super Eagles,kama mwenzake mjerumani Ottmar Hitzfeld, kocha wa Uswisi, alivyowanasa jana mabingwa wa ulaya,Spain ? Mbinu pekee ikawa ni kushambulia.Ugiriki ilifuta kwanza madhambi ya kutotia bao katika Kombe la dunia tangu 1994.

Nigeria, ilianza bila ya washambulizi wake wanaotamba katika Bundesliga-Cheudu Obasi wa Hoffenheim na Obafemi Martin wa Wolfsburg.Ilibainika baadae,hawahitaji washambulizi,bali walinzi. Taiwo na Yakubu lakini,wakizima hujuma za wagiriki.

Ikiongoza kwa bao 1 hadi dakika ya 33 ya mchezo ,mkondo wa mchezo uliwageukia Nigeria, pale Sani ,alipotimuliwa nje ya uwanja kwa kucheza ngware. Nigeria, ilibakiwa na saa nzima kuzima hujuma za wagiriki.Msiba ulioikumba Bafana bafana masaa 24 kabla kwa kutimuliwa nje kwa kipa wake,ukaikumba pia Nigeria. wakati huu, jahazi la Nigeria, linaenda mrama,ingawa bado kuzama.Gekas, mshambulizi wa wagiriki,akipiga sana hodi langoni mwa Super Eagles.Nigeria,wamshukuru Enyama kwenda mapumzikoni bila wagiriki kusawazisha.lakini ilikua swali la wakati tu lini hujuma za wagiriki zitafua dafu.

Kabla ya Nigeria na Ugiriki kuingia uwanjani, Kikosi cha Maradona,Argentina kikitamba na Lionel Messi na Higuain,kilikuwa cha kwanza kukata tiketi yake ya duru ijayo kilipoitimua nje Korea ya kusini kwa mabao 4:1. Mabao yangelikuwa hata mengi zaidi laiti,si kipa wa Korea Kusini.Bao lao wenyewe katika lango lao alilopachika Park Chu Young,mnamo dakika ya 17 ya mchezo, lilikuwa kaburi lilikuja mwishoe, kuwazika Johannesberg .

Kwani, lilifuatiwa na mabao 3 maridadi ajabu aliotia Gonzalo Higuain-hattrick. Kwanza , alipiga hodi dakika ya 33 ya mchezo.Utamu ulipomkolea wa kutia mabao, Higuain,alirdi kupiga hodi tena katika lango la wakorea mnamo dakika ya 76 ya mchezo na kila akikaribishwa ndani,alirudi tena mara ya mwisho dakika ya 80 kwa bao lake la 3 na la 4 kwa Argentina. Dakika 1 kabla firimbi ya mapumziko, Lee Yong, alilifumania lango la Argentina kwa bao lao la kufuta machozi baada ya uzembe wa mlinzi wa Argentina, Demecheli. Lionel Messi, alinawiri kwa chenga na pasi zake maridadi,ingawa binafsi bado hakutia bao. Argentina,imeshatangulia duru ijayo bila kujali Wagiriki , wanigeria na wakorea kusini, watamalizana vipi.

Baada ya Nigeria na Ugiriki kuondoka uwanjani,itakua zamu ya makamo-bingwa wa dunia-Le Blue-Ufaransa ,kutamba na akina Riberry,Malouda na Thierry Henry,kudai pointi 3 kutoka Mexico. Mexico ilianza sare na Bafana Bfana ijumaa iliopita zilipoachan sare bao 1:1.Uruguay, ambayo jana ilizima mazumari ya vuvuzela ya Afrika Kusini, inatumai Mexico itawatoa nje wafaransa ili ndugu 2 wa Amerika Kusini,wajiunge mwishoe na Argentina na Brazil duru ijayo.

Ufaransa, haimudu kushindwa mpambano huu wa usiku wa leo.

Mwandishi: Ramadhan Ali / DPAE

Uhariri: Abdul-Rahman