1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Obama au Clinton, McCain au Romney?

Dreyer, Maja5 Februari 2008

Wajumbe wa vyama vya Demokratik na Republican leo katika siku inayoitwa "Super Tuesday" nchini Marekani wanapiga kura kuwateua wagombea kiti cha urais.

https://p.dw.com/p/D30F
Hillary Clinton katika kampeni yakePicha: AP
Kila ukiwasha televisheni au redio siku ya leo nchini Marekani, mada inayozungumziwa ni moja tu, yaani uchaguzi katika majimbo 24 wa kuwachagua wawakilishi wa vyama watakaohudhuria mikutano ya uteuzi ya wagombea wa kiti cha urais. Katika chama cha Republikan, wanaoongoza kwa sasa ni John McCain, seneta wa jimbo la Arizona, na Mitt Romney, gavana wa zamani wa jimbo la Massachusetts. Katika kampeni zao za mwisho, wagombea hao wawili walijaribu kuwashawishi wafuasi kwa kila mmoja kujidai kuwa mhafidhina kuliko mwingine. Anayebakia pia katika shindano la chama cha Republikan ni gavana wa zamani wa jimbo la Arkansas, Mike Huckabee.
Lakini macho ya dunia nzima yanaangaza zaidi katika mvutano baina ya wajumbe wa chama cha Demokratik wakiwa ni seneta wa Illinois, Barack Obama na seneta wa New York, Bi Hillary Clinton. Tangu kampeni zilipoanza, Barack Obama anazidi kuungwa mkono na wapigaji kura. Mwanasiasa huyu baba yake akiwa Mkenya ana uwezo wa kuwavutia watu. Ujumbe wake ni mmoja hasa kwamba sasa wakati umewadia wa kuleta mabadiliko.

O-Ton Obama:
"Tunapopambanishwa na kebehi wasiwasi na hofu, tukiambiwa kwamba hatuna uwezo, basi tunajibu katika msingi wa imani ya watu wa Marekani kwa kusema: ndiyo tunaweza."
Mpinzani wake lakini, Bi Clinton ni mtu mwenye uzeofu wa miaka 35 katika masuala ya kisheria na siasa. Katika kampeni hizo ambazo zilitumia fedha nyingi zaidi tangu uchaguzi kufanyika nchini Marekani, Bibi huyu mke wa aliyekuwa rais Bill Clinton ametoa ahadi ifuatayo:
O-Ton Clinton: "Ikiwa mtanichagua nitaamka kila siku kufanya kile nilichoahidi. Sina haja ya kuazimwa imani, ninawaomba mnichague ili nitimize kazi yenye dhamana kubwa kuliko zote duniani."
Wasaidizi wa wagombea wote wawili wa chama cha Demokratik sasa wanapuuza matumaini kwamba uchaguzi wa leo utaleta matokeo ya mwisho. Leo, zaidi ya nusu ya wawakilishi wa chama cha Demokratik wataamuliwa pamoja na asilimia 40 ya wajumbe wa Republikans.Wagombea wote wanapigania hasa majimbo yenye wajumbe wengi kwa mikutano ya vyama kama California na majimbo ya Kaskazini Mashariki. Mifumo ya uchaguzi wa vyama hivi lakini inatofautiana. Wademokrats wanatumia uwakilishi unaofanana na kura wakati mgombea wa Republikan akishinda katika jimbo fulani anapata kura zote. Ndiyo sababu kwa upande wa chama cha Demokrativ, ushindano kati ya Barack Obama na Hilary Clinton unaendelea kupishana chupu chupu.