1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Obama awatahadharisha wapiga kura kuhusu Trump

3 Novemba 2016

Rais Barrack Obama amewahimiza wafuasi wa chama cha Democratic kumpigia kura Hillary Clinton na kuonya kwamba Donald Trump ni tishio kwa haki za kijamii, taifa la Marekani na dunia nzima kwa ujumla.

https://p.dw.com/p/2S5Ac
USA | Auftritt US-Präsident Barrack Obama auf der Wahlkampfveranstaltung in Miami Gardens
Picha: Getty Images/J. Skipper

Rais wa Marekani Barrack Obama amewahimiza wafuasi wote wa chama cha Democratic kumpigia kura kwa wingi Hillary Clinton siku ya uchaguzi wiki ijayo na kuonya kwamba Donald Trump mgombea urais wa chama cha Republican ni tishio kwa haki za kijamii ambazo ziliafikiwa kupitia hali ngumu , taifa la Marekani na dunia nzima kwa ujumla.

Akigusia chaguo la rais siku ya Jumanne wiki ijayo, rais Barrack Obama alimpuuzilia mbali Trump kuwa mtu asiyestahili kabisa kuwa rais.

Kufikia sasa Clinton bado anaonyesha uwezekano wa kuwa rais wa 45 wa Marekani lakini huku zikiwa zimesalia siku sita kabla ya uchaguzi huo mkuu, wafuasi wa chama cha Demokratic bado wako chonjo hasa kutokana na mienendo ya Trump isiyotabirika.

Obama aliwaambia wapiga kura katika mji wa Chapel Hill kuwa hatima ya taifa hilo imo mikononi mwao . Aliongeza kwa kusema, „"hatima ya dunia inawategemea nyinyi, wapiga kura wa North Carolina itawabidi kuhakikisha munachukuwa hatua katika mwelekeo bora."

USA Iowa Präsidentschaftskandidatin Hillary Clinton
Mgombea wa chama cha Democratic Hillary ClintonPicha: Reuters/B. Snyder

Wikileaks yaendelea kutoa barua pepe

Huku kampeini hizo zikipamba moto, barua pepe nyingine za siri zinazomhusu Hillary Clinton zilitolewa hapo jana na mtandao wa wikileaks unaofanya udukuzi na kuchapisha taarifa za siri, hizi zikiwa sehemu ya barua pepe zinazotolewa na mtandao huo kila siku tangu mwezi uliopita.

Mtandao huo umesema kuwa unanuia kutoa barua pepe hizo zilizoibwa kutoka kwa akaunti ya mkuu wa kampeini ya Hillary Clinton , Podesta kila siku katika kipindi hiki cha uchaguzi.

Hata hivyo msemaji wa wizara ya mashauri ya kigeni ya Marekani John Kirby alisema hapo jana kuwa wizara hio haitatoa taarifa yoyote kuhusiana na madai hayo ya stakabadhi zilizoibwa lakini akasema kuwa juhudi za wizara hiyo za kutoa taarifa sahihi kwa vyombo vya habari kuhusiana na kipindi cha kuhudumu kwa Hillary katika wizara hiyo mara nyingine ilihitajika kuwasiliana na waakilishi wake kuhakikisha kuwepo kwa usawa.

Kundi la kampeini la Clinton hata hivyo limekuwa likionya kuwa mtandao huo wa wikileaks umeharibu barua pepe zilizoibwa na wadukuzi ambao huenda wanafanyia kazi serikali ya Urusi.

 

Mwandishi: Tatu Karema/ AP/ APE

Mhariri: Iddi Ssessanga