1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Obama ayalaani mashambulio ya mabomu mjini Kampala.

Halima Nyanza14 Julai 2010

Rais Barack Obama amelaani shambulio la mabomu lililofanywa mjini Kampala na kuua watu wengi na kuwawaonya Waafrika juu ya makundi ya siasa kali kama al Qaeda kwamba yamekuwa hayajali maisha ya watu wasio na hatia.

https://p.dw.com/p/OIjf
Rais Barack Obama wa Marekani amelilaani shambulio la bomu lililofanywa mjini Kampala na wapiganaji wa al Shabaab.Picha: AP

Rais Obama ameyasema hayo  ikiwa ni changamoto yake binafsi kwa makundi ya watu wenye msimamo mkali juu ya bara la Afrika baada ya shambulio lililotokea nchini Uganda, ambalo wapiganaji wenye msimamo mkali kutoka Somali walikiri kuhusika.

Akizungumza na Shirika la Utangazaji la Afrika kusini -SABC-, Rais Barack Obama, amesema baadhi ya taarifa zilizotolewa na makundi hayo ya kigaidi, zinaonesha kutojali maisha ya Afrika kama kitu chenye thamani, na kuona kuwa kama sehemu yenye uwezekano wa kufanya mapambano ya kiitigadi, ambayo yanaua watu wasio na hatia bila ya kujali matokeo yake katika kipindi kirefu kwa ajili ya kufaidika kwao kwa kipindi cha muda mfupi.

Kauli hiyo aliyoitoa Rais Obama katika mahojiano yake na shirika hilo la utangazaji la Afrika kusini ni ya kwanza kuitoa, kuhusiana na shambulio la mabomu lililotokea Jumapili iliyopita mjini Kampala Uganda.

Rais wa Marekani ameelezea wasiwasi wake kuhusiana na kundi lolote, hususan ambalo linamafungamano na al Qaeda, hasa juu ya uwezekano wa kufanya mashambulio nje ya eneo hilo.

Soldaten der Al-Shabab-Miliz vor Mogadischu
Kundi la wapiganaji wa al-Shabab lililokiri kuishambulia Uganda.Picha: AP

Aidha amesema ni huzuni kuona kuwa mlipuko kama huo unatokea wakati watu barani Afrika wanasherehekea na kuangalia mashindano ya kombe la dunia la soka, yaliyokuwa yakifanyika Afrika kusini na kwamba siku shambulio hilo likitokea ilikuwa ni mchezo wa fainali kati ya Uholanzi na Hispania.

Uganda Anschlag Bombe Juli 2010
Mmoja wa raia wa Marekani aliyejeruhiwa katika shambulio la bomu mjini Kampala Uganda.Picha: picture-alliance/dpa

Wapiganaji wa al Shabaab wa Somalia, ambao waliokiri kufanya shambulio hilo, wamesema wamefanya hivyo kwa ajili ya kulipiza kisasi ya kuwepo kwa vikosi vya majeshi ya Uganda mjini Mogadishu.

Kwa upande wake Afisa wa ngazi za juu wa serikali ya Marekani ambaye hakutaka kutaja jina lake, ameushutumu mtandao wa kigaidi wa al Qaeda, wenye mafungamano na kundi lililokiri kufanya mashambulio yazo ya kampala la al Shabaab, kuwa ni wa kibaguzi ambalo linatishia Waafrika weusi na kwamba halithamini maisha ya binadamu.

Maafisa wa serikali ya Marekani pia wamelinganisha mashambulio hayo yaliyofanywa nchini Uganda na yale yaliyotokea katika ubalozi wa Marekani katika nchi za Kenya na Tanzania, ambapo liliua maelfu ya waafrika, na wameonya kuwa  al Qaeda inawaangalia watu katika bara hilo kama chambo cha mafanikio yao.

Aidha wamesema pia watafiti wa masuala ya kijasusi wa Marekani wamefahamisha kuwa  baadhi ya viongozi wa al Qaeda wamekuwa wakiwalenga Waafrika kuja kuwa wafanya mashambulio ya kujitoa mhanga kwa siku za baadaye.

Shambulio hilo la mwishoni mwa wiki mjini Kampala ni la kwanza kufanywa na wapiganaji hao wa al Shabaab nje ya Somalia.

Mwandishi: Halima Nyanza(afp)

Mhariri:Abdul-Rahman