1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Obama katika ziara ya mwisho kama rais Ujerumani

24 Aprili 2016

Rais Barack Obama wa Marekani ameanza ziara ya siku mbili Ujerumani Jumapili (24.04.2016) akitaraji kuondowa mashaka mazito ya umma kuhusu makubaliano ya biashara huru kati ya Marekani na Ulaya.

https://p.dw.com/p/1IbpN
Rais Barack Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani katika Kasri la Herrenhausen mjini Hannover. (24.04.2016)
Rais Barack Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani katika Kasri la Herrenhausen mjini Hannover. (24.04.2016)Picha: Reuters/K. Pfaffenbach

Kansela Angela Merkel alimkaribisha Obama kwa mapokezi makubwa kwa kile yumkini ikawa ndio ziara yake ya mwisho kama rais nchini Ujerumani ambapo ametandikiwa zulia jekundu katika Kasri la Herrenhausen makaazi ya zamani ya kifalme wakati wa majira ya kiangazi yaliojengwa upya baada ya kubomolewa katika Vita Vikuu vya Pili vya Dunia.

Baada ya kukaguwa gwaride la heshima la vikosi vya Ujerumani katika bustani ya kasri hilo Obama alikutana na Merkel katika mazungumzo ya faragha.

Akizungumza katika mkutano wa pamoja na waandishi wa habari uliohudhuriwa pia na Merkel, Obama Marekani na Umoja wa Ulaya zinapaswa kuendelea kushinikiza kufikiwa kwa makubaliano ya biashara huru kati ya Marekani na Ulaya licha ya upinzani mkubwa dhidi ya makubaliano hayo.Amesema Angela na yeye wamekubaliana kwamba Marekani na Umoja wa Ulaya zinatakiwa kusonga mbele mazungumzo ya Biashara kati ya Marekani na Ulaya na Ushirikiano wa Uwekezaji. Pia amesema ni jambo lisilokuwa na ubishi kwamba biashara hiyo huru imeimarisha uchumi wa Marekani na pia kuleta faida kubwa kwa nchi zinazohusika na biashara hiyo.

Merkel mshirika wa kuaminika

Katika suala la Syria Obama amesema itakuwa vigumu sana kuona vipi kile kinachojulikana kama kanda salama kinavyoweza kutekelezwa nchini Syria bila ya kujitolea kijeshi kwa kiwango kikubwa sana.

Deutschland Hannover Besuch Obama und Merkel
Rais Barack Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani katika Kasri la Herrenhausen mjini Hannover. (24.04.2016)Picha: Reuters/K. Pfaffenbach

Amesema suala kuhusiana na kanda hiyo ndani ya ardhi ya Syria sio la kupinga kiitikadi kwa upande wake " Sio suala kwamba mimi sitaki ningeliweza kusaidia kulinda umma mkubwa wa watu.Ni suala la utekelezaji hasa juu ya vipi unaweza kulitekeleza ?"

Obama pia ametumia fursa hiyo kumpongeza Kansela Angela Merkel wa Ujerumani kuwa ni "mshirika muaminifu" na kuelezea jinsi anavyoshughulikia mzozo wa wakimbizi kuwa ni "ushujaa". Obama amesema Merkel ni "rafiki na mshirika " na kwamba ni mshirika wa kuaminika ambaye maamuzi yake anayathamini.

Kwa upande wake Merkel akizungumzia suala la Ukraine amesema usitishwaji wa mapigano mashariki mwa Ukraine hauko imara na kwamba yeye na Obama wamezungmzia njia za kuhakikisha makubalino ya amani ya Minsk yanatekelezwa.

Masuala ya kujadiliwa

Juu ya kwamba mada kuu ya Obama katika ziara yake hiyo ni suala la Biashara kati ya Marekani na Ulaya na Ushirikiano wa Uwekezaji masuala mengine hayawezi kupuuzwa kama vile juhudi za kupambana na kundi la Dola la Kiislamu,kuimarisha ushirikiano wa kupambana na ugaidi na kuzishajiisha nchi kushirikiana taarifa za mashirika ya ulinzi na usalama.

Rais Barack Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani katika mkutano wa pamoja na waandishi wa habari lmjini Hannover. (24.04.2016)
Rais Barack Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani katika mkutano wa pamoja na waandishi wa habari lmjini Hannover. (24.04.2016)Picha: picture-alliance/dpa/K.Nietfeld

Kundi la Dola la Kiislamu limedai kuhusika na mashambulizi yaliofanyika Brussels mwezi uliopita na kuuwa zaidi ya watu 30.Katika ziara hii Obama pia anataka kuonyesha hadharani uungaji mkono wake kwa ushujaa wa Merkel kushughgulikia mzozo wa wahamiaji.

Uamuzi wake wa kuruhusu maelfu ya wakimbizi wanaokimbia vita nchini Syria kupatiwa makaazi mapya nchini mwake umezusha tafrani ya umma dhidi yake.Hivi karibuni Merkel amesaidia nchi za Ulaya kufikia makubaliano na Uturuki kupunguza wimbi la wakimbizi wanaoingia katika nchi hizo lakini sasa yeye pamoja nba viongozi wengine wa Ulaya wanakabiliwa na shinikizo la kutathmini upya makubaliano hayo.

Kibaruwa kigumu

Obama anakabiliwa na kibaruwa kigumu kupigia debe makubaliano ya biashara kati ya Ulaya na Marekani yanayojulikana kama TTPI hususan nchini Ujerumani.

Baadae Jumapili Obama anaungana na Merkel kufunguwa maonyesho ya viwanda na biashara ya Hannover ambayo ni maonyesho makubwa kabisa ya teknolojia ya biashara duniani na kuyanadi makubaliano hayo.

Maelfu ya watu waliingia mitaani hapo Jumamosi mjini Hannover siku moja kabla ya kuwasili kwa Obama. Baadhi walikuwa wamebeba mabango kuigiza kauli mbiu ya Obama wakati wa kampeni ya urais mwaka 2008 "Ndio tunaweza -Komesha TTIP".Hapo mwezi wa Novemba zaidi ya watu 100,000 waliandamana mjini Berlin kupinga makubaliano hayo yanayopendekezwa.

Rais Barack Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani katika bustani ya Kasri la Herrenhausen mjini Hannover. (24.04.2016)
Rais Barack Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani katika bustani ya Kasri la Herrenhausen mjini Hannover. (24.04.2016)Picha: Reuters/K. Pfaffenbach

Wanaotetea makubaliano hayo wanasema yatakuza biashara wakati kukiwa na hali ya wasi wasi wa kiuchumi duniani. Wale wanaoyakosowa wanahofia kumomonyoka kwa hatua za kuwalinda walaji na viwango vya kuhifadhi mazingira.

Wajumbe huko Washington na Ulaya wanajaribu kukamilisha vifungu vya mwisho vya makubaliano hayo kabla ya kumalizika kwa mwaka huu ambapo baada ya hapo mtu atayechukuwa nafasi ya Obama na kampeni za uchaguzi barani Ulaya katika nchi kubwa za Ulaya vinaweza kuzidi kukwamisha mazungomzo ambayo tayari ni magumu.

Hapo Jumatatu Obama ataungana na Merkel kutembelea maonyesho ya biashara na kutowa hotuba kuhusu changamoto inazozikabili Marekani na Ulaya. Merkel pia ataitumia fursa hiyo kwa kuwaalika viongozi wa Uingereza, Ufaransa na Italia huko Hannover kwa mkutano kujadili Syria,Libya,kundi la Dola la Kiislamu,uhamiaji na masuala mengine.

Mwandishi : Mohamed Dahman/AP

Mhariri : Abdu Mtulya