1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Obama, Romney wachuana katika mdahalo

4 Oktoba 2012

Wagombea kiti cha Urais wa Marekani Rais Barack Obama na mwenzake Mitt Romney wamefanya mdahalo wao wa kwanza kupitia televisheni ambao umewaacha wengi na mshangao kutokana na kwenda kinyume na matarajio yao.

https://p.dw.com/p/16JZT
Barak Obama na Mitt Romney Denver USA
Barak Obama na Mitt Romney Denver USAPicha: Reuters

"Miaka minne iliyopita niliposimama katika jukwaa hili nilisema kuwa nitapunguza kodi kwa familia zenye kipato cha kati. Na hivyo ndivyo nilivyofanya. Tumepunguza kodi kwa familia za kipato cha kati kwa kiasi cha dola 3600. Na sababu ni kuwa naamini tutakuwa na mafanikio kama watu wa kipato cha kati watakuwa na mafanikio"

Hivyo ndivyo alivyoanza mazungumzo Rais Obama katika mjadala huo uliofanyika Chuo Kikuu cha Denver mjini Colorad na kutazamwa moja kwa moja kupitia televisheni na watazamaji wanaokadiriwa kufikia milioni 50.

Rais Barak Obama akizungumza katika mdahalo wa Denver Colorado, Marekani
Rais Barak Obama akizungumza katika mdahalo wa Denver Colorado, MarekaniPicha: Reuters

Obama alizungumza kwa muda mrefu lakini mpinzani wake Romney alimkosoa zaidi kwa namna anavyoendesha utawala wake jambo ambalo lilionekana kumgusa. Mkurugenzi wa kituo cha siasa na masuala ya umma Terry Madonna anasema kuwa Obama hakuwa katika hali yake ya kawaida hivyo hakufanya vile ambavyo wafuasi wake na watu wengine duniani walivyotarajia.

Romney alimshambulia kwa Rais Obama juu ya histora yake ya kushughulikia matatizo ya kiuchumi lakini safari hii hakuropoka wala kutoa matamshi ya kutatanisha kama alivyozoeleka.

Mashambulizi ya Romney

Romney alitumia mtindo wa kushambulia na kisha kurejea katika nukta zake akionyesha namna atakavyoshughulikia kila kosa la Obama alilolionyesha. Wachambuzi wanasema kuwa Romney ameweza kumbwaga mpinzani wake katika awamu hiyo ya kwanza ya mdahalo.

"Sina shaka akilini mwangu kuwa kama rais atachaguliwa tena mtaendelea kuona watu wa kipato cha kati wakishuka zaidi huku kipato kikipungua na bei zikipanda juu. Nitainua kipato tena. Tuna ukosefu wa ajira wa asilimia nane zaidi mwezi huu na kama nikiwa rais nitatoa nafasi mpya za ajira milioni 12 kwa nchi hii", alisema Romney.

Kwa upande wa masuala ya afya Romney aliuponda mpango wa afya, maarufu kama Obamacare, wenye thamani ya dola za Marekani trilioni 2.8 na kusema haufai lakini hakuweza kuja na mbadala sahihi kwa wapigakura.

Mitt Romney mgombea wa Republican akizungumza katika mdahalo
Mitt Romney mgombea wa Republican akizungumza katika mdahaloPicha: Reuters

Masuala ya afya ni moja kati ya ajenda kuu kuelekea uchaguzi wa Novemba 6 mwaka huu. Mpango wa huduma za afya wa Marekani ndio wenye gharama zaidi kuliko nchi zote na unalaumiwa kuwa kuchangia katika kushuka kwa mishahara ya Wamarekani.

Romney kinara uchunguzi wa maoni ya mdahalo

Uchunguzi wa maoni uliofanywa na kituo cha televisheni cha CNN kwa watu wenye umri wa kupiga kura na walioangalia mdahalo huo unaonyesha kuwa Romney amepata asilimia 67 huku Obama akiambulia asilimia 25. Uchunguzi kama huo umefanywa pia na kituo cha televisheni cha CBS na Romney amepata ushindi.

Mgombea mwenza wa Obama, Joe Biden
Mgombea mwenza wa Obama, Joe BidenPicha: dapd

Huu ni mdahalo wa kwanza kati ya mitatu iliyopangwa kufanyika. Wagombea wenza kutoka pande zote mbili watakutana pia kwa mdahalo wiki ijayo. Watu wanasubiri kuona nini kitajiri kati ya mgombea mwenza wa Obama Joe Biden kutoka chama cha Democrat na yule wa Romney Paul Ryan kwa tiketi ya chama cha Republican

Mhariri: Stumai George/Reuters/afp

Mwandishi: Mohammed Khelef