1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Olmert,Abbas kufanya mazungumzo zaidi.

Charles Mwebeya19 Februari 2007

Mkutano uliofanyika leo kati ya Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Bi Condoleeza Rice na Waziri Mkuu wa Israel Ehud Olmert , pamoja na Rais wa mamlaka ya Palestina Mahmud Abbas umemalizika huku pande zote zikikubaliana kuendelea na mazungumzo zaidi ya kuleta amani katika eneo la mashariki ya kati.

https://p.dw.com/p/CHJx
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Bi. Condoleeza Rice (katikati)katika picha ya pamoja na Rais wa mamlaka ya Palestina Mahmud Abbas (kushoto) na Waziri mkuu wa Israel Ehud Olmert.
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Bi. Condoleeza Rice (katikati)katika picha ya pamoja na Rais wa mamlaka ya Palestina Mahmud Abbas (kushoto) na Waziri mkuu wa Israel Ehud Olmert.Picha: AP

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya mkutano huo, Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Bi. Condoleeza Rice amesema pande zinazohusika katika mazungumzo hayo zimekubaliana kukutana tena hivi karibuni.

Katika taarifa ya saa moja unusu aliyoitoa mbele ya waandishi wa habari, Bi. Rice amesema Rais Mahmud Abbas pamoja na Waziri mkuu wa Israel walibadilishana mawazo juu ya hali ya baadaye ya kisiasa katika eneo hilo na kukubali kukutana tena hivi karibuni.

Pia katika mazungumzo hayo, viongozi hao walizungumzia masuala mbalimbali juu ya uundwaji wa serikali ya umoja wa kitaifa ya mamlaka ya Palestina na utayari wa serikali ya Palestina kudhibiti ghasia ,pamoja na kuitambua Israel kama taifa .

Si Rais Abbas wala Waziri Mkuu Ehud Olmert alieyeandamana na Waziri huyo wa mambo ya nje wa Marekani katika mkutano na waandishi wa habari, ambapo pia waandishi wa Habari hawakupewa nafasi ya kuuliza maswali.

Vile vile maofisa wa Israel na Palestina hawakuwa tayari kuzungumzia lolote juu ya mkutano huo.

Kabla ya kuanza kwa mkutano huo, Bi. Rice ,Waziri mkuu wa Israel Ehud Olmert pamoja na Rais wa mamlaka ya Palestina Mahmud Abbas walipiga picha ya pamoja.

Kwa mujibu wa taarifa ya Bi. Rice ni kwamba viongozi hao wamekubali kurejea katika mazungumzo ya Road Map , huku Bi Rice akisisitiza kurejea katika eneo hilo la mashariki ya kati mapema iwezekanavyo.

Mkutano huo ulichukuliwa kama juhudi za Marekani kuimarisha mazungumzo ya amani kati ya Israel na Palestina kufuatia makubaliano ya makundi ya Hamas na Fatah ya mwezi huu huko Macca ya uundwaji wa serikali ya umoja wa kitaifa ya mamlaka ya Palestina

Mazungumzo hayo ya leo yamefanyika huku zikiwa zimesalia wiki tano kwa Bunge la palestina kuidhinisha baraza la mawaziri la chini ya waziri mkuu wa Ismail Haniya.

Kama ilivyotarajiwa mazungumzo ya leo hayakutoa ufumbuzi wa moja kwa moja wa matatizo ya eneo la mashariki ya kati.

Hapo jana Wapalestina wengi walichukizwa na kauli iliyotolewa na Waziri mkuu wa Israel Ehud Olmert kuwa Rais Bush tayari amekubali kuungana na Israel kuitoitambua serikali ya Palestina mpaka kundi la Hamas linalounda serikali ya mamlaka ya Palestina litakapokubali kuitambua Israel na kukomesha ghasia.

Kauli hiyo ya Olmert ilichukuliwa na wapelestina wengi kama ni hatua ya kufifisha mazungumzo ya amani katika eneo hilo la Mashariki ya kati.