1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

OPEC kuanza mkutano leo mjini Riyadh

Tuma Provian Dandi16 Novemba 2007

Suala la mabadiliko ya hali ya hewa linatarajia kupewa kipaumbele katika mkutano wa nchi zinazozalisha mafuta kwa wingi diniani OPEC

https://p.dw.com/p/CIle
Rais wa OPEC Sheikh Ahmed Fahed al-Sabah, ambaye pia ni Waziri wa Nishati wa Kuwait
Rais wa OPEC Sheikh Ahmed Fahed al-Sabah, ambaye pia ni Waziri wa Nishati wa KuwaitPicha: dpa - Report

Agenda ya kukabiliana na mabadiliko makubwa ya hali ya hewa ni moja na mambo yanayotarajiwa kuzungumzwa katika mkutano wa mataifa wanachama wanaozalisha mafuta kwa wingi-OPEC unaoanza leo mjini Riyadh katika Falme za Kiarabu.

Hata hivyo Mawaziri wa Nishati kutoka nchi zinazozalisha mafuta kwa wingi duniani wamesema sera ya kuzalisha mafuta kwa wingi haitakuwemo katika mkutano huo, badala yake suala hilo litajadiliwa katika mkutano mwingine utakaofanyika tarehe tano Desemba huko Abu Dhabi.

Awali, maofisa kutoka Muungano huo, wataalamu wa uchumi na Mawaziri wa Mambo ya Nje kutoka nchi wanachama, walipata nafasi ya kuandaa taarifa zitakazowakisilishwa kwenye mkutano.

Mmoja wa washiriki ambaye hakutaka kutoa jina lake amesema malengo watakayozungumza siyo ya muda mfupi, na kwamba yatazama katika kukabiliana na kitisho cha kuongezeka kwa joto duniani.

Suala jingine linalotarajia kuwasilishwa katika mkutano wa leo ni mipango ya muda mrefu itakayoiwezesha OPEC kumudu shughuli zake za kuzalisha nishati ya mafuta, pamoja na haki ya usalama kwa bidhaa zinazozalishwa na washirika hao.

Waziri wa Nishati na Madini wa Algeria Bwana Chakib Khelil amewambia waandishi wa habari kwamba nchi wanunuzi pia wanahitaji kutimiziwa ubora na usalama wa bidhaa wanazonunua, ili kuepuka mizozo inayoweza kujitokeza.

Naye Waziri wa Nishati wa Venezuela Rafael Ramirez, amesema pia ni muhimu kwa mkutano wa Riyadh kuzungumzia udhaifu dhidi ya dola ya Marekani, kwa vile pia imechangia kupanda kwa gharama za mafuta hali inayowafanya watu wengi duniani kutaabika.

Utafiti unaonesha kwamba katika robo ya tatu ya mwaka huu nishati ya mafuta imekuwa pungufu kwa karibu asilimia 2, japo Venezula inasema kwamba bado kuna kiasi kikubwa cha mafuta sokoni.

Wakati Vezuela ikitoa kauli hiyo, Marekani ina ziada ya mapipa milioni 2.8 ya mafuta ghafi katika soko la ndani kiasi kitakachoisaidia wakati wa kipindi hiki cha baridi.

Katika mkutano huo wa OPEC wa mjini Riyadh, Mawaziri wa Mafuta na Nishati kutoka nchi wanachama wamekusudia kulizungumzia kwa undani suala la mazingira kwa vile shughuli za uzalishaji wa mafuta huchangia kuongeza hali ya joto duniani, wakitumaini kwamba wana nafasi kubwa katika hilo.

Katibu Mkuu wa OPEC Bwana Abdullah Al Khalid amekaririwa akisema kwamba wako tayari kununua teknolojia mpya inayoweza kudaka hewa ya kaboni dayoksaidi na kuihifadhi, ili kupunguza madhara kwa mabadiliko ya hali ya hewa.

Teknolojia hiyo itawezesha kuzika hewa hiyo ardhini, badala ya kusambaa angani ambako inaongeza joto duniani.

Uchunguzi unaonesha kwamba nchi wanachama wanaozalisha nishati ya mafuta OPEC, zinazalisha robo tatu ya mafuta yote yanayotumika duniani.