1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ataka demokrasia kuheshimiwa katika mataifa mengine

Sylvia Mwehozi17 Mei 2016

Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani Papa Francis ameyakosoa mataifa ya Magharibi kwa kulazimisha demokrasia yake kuenea katika mataifa mengine pasipo kuheshimu asili ya siasa za wazawa.

https://p.dw.com/p/1Iozt
Vatikan Papst Franziskus hält Pfingsrede vor dem Petersdom
Picha: picture-alliance/dpa/S. Spaziani

Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani Papa Francis ameyakosoa mataifa ya Magharibi kwa kutaka kuiuza aina ya demokrasia yake kwa mataifa mengine pasipo kuheshimu asili ya siasa za wazawa, huku akipongeza kuchaguliwa kwa meya wa kwanza Muislamu jijini London.

Katika mahojiano hayo na gazeti la Kanisa Katoliki la nchini Ufaransa La Croix , Papa Francis amesema Ulaya inapaswa kuunganisha vyema suala la wahamiaji na kampeni ya kusambaza kile kinachoitwa demokrasia ya Kimagharibi kwenye mataifa wanakotoka wakimbizi hao.

Papa Francis ameliambia gazeti hilo na hapa namnukuu: "Kulingana na kitisho cha ugaidi wa Kiislamu, tunapaswa kuhoji namna demokrasia ya mataifa ya Ulaya ilivyopelekwa katika mataifa ambayo yalikuwa na nguvu, kama nchini Iraq au Libya, ambako kulikuwa na muundo mzuri wa kikabila." Mwisho wa kunukuu.

Ameongeza kwamba hakuna hatua zinazoweza kupigwa pasipo kuzingatia tamaduni hizo. Akitolea mfano siasa za Libya, Papa Francis anasema "kama Walibya walivyosema hivi karibuni, tulikuwa na Gaddafi mmoja ila sasa wapo 50", akirejelea rais wa zamani wa taifa hilo, Muammar Gaddafi, ambaye aliondolewa madarakani na kuuawa mwaka 2011.

Mara kadhaa kiongozi huyo wa Kanisa Katoliki amekuwa akishambulia kile anachokiita "ukoloni wa kitamaduni" ambapo mataifa yaMmagharibi yanalazimisha maadili yake kuenea katika mataifa yanayoendelea kwa malipo ya misaada ya kifedha.

Wakimbizi kutokea nchini Libya
Wakimbizi kutokea nchini LibyaPicha: picture alliance/dpa/Str

Amesema suala la wakimbizi wa "maghetto" halikuwa baya, lakini limepotoshwa katika mapambano dhidi ya ugaidi.

Ametolea mfano wa shambulizi la bomu la mjini Brussels la mwezi Machi kuwa magaidi hao walikuwa ni raia wa Ubelgiji, wakiwa ni watoto wa wahamiaji waliokulia katika maghetto.

Katika hatua nyingine, Papa Francis amepongeza kuchaguliwa kwa Sadiq Khan kama meya wa kwanza Muislamu wa jiji kubwa la London nchini Uingereza. Anasema kuwa na hapa nanukuu "Jijini London, meya mpya aliapishwa katika Kanisa Kuu na pengine alipokelewa na Malkia. Hii inaonyesha umuhimu wa Ulaya kurejesha uwezo wake wa kushirikiana." Mwisho wa kumnukuu.

Siku 10 zilizopita Papa Francis aliyakosoa tena mataifa ya Ulaya kwa kutoa majibu yasiyoridhisha juu ya utitiri wa wahamiaji wanaokimbia vita na umaskini Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini.

Mwandishi: Sylvia Mwehozi /RTRE

Mhariri: Mohammed Khelef