1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Papa kuongoza Ibada ya kwanza ya Ijumaa Kuu

29 Machi 2013

Papa Francis Ijumaa(29.03.2013) anaongoza ibada yake ya kwanza ya Ujumaa Kuu ya Pasaka baada ya kuosha miguu ya wafungwa 12 vijana akifuata taratibu za kale katka juhudi za kulisogeza Kanisa Katoliki karibu na maskini.

https://p.dw.com/p/186yJ
Papa Francis
Papa FrancisPicha: Reuters

Papa huyo mpya anatarajiwa kusoma hadithi ya "Mateso ya Yesu Kristo" ambayo ni hadithi inayohusu muda wa mwisho wa maisha ya Yesu katika Kanisa la Mtakatifu Peter kabla ya kuongoza msafara wa ibada ya kufuata njia alizopita Yesu wakati akisulubiwa mslabani ambapo maelfu ya Wakristo inaaminika kuwa waliuwawa wakati wa utawala wa Warumi.Francis ambaye siku zake za mwanzo akiwa kama papa zimeonyesha tafauti kubwa na mtangulizi wake Benedikt wa kumi na sita anatarajiwa kushiriki katika maandamano hayo na hata kubeba msalaba wa mbao begani mwake wakati fulani wa msafara huo.Mwaka jana Benedict aliekua dhaifu mwenye umri wa miaka 85 aliangalia tu ibada hiyo.

Papa aosha miguu ya wafungwa

Papa  mpya pia alifanya utaratibu wa ibada ambao haukuwahi kufanyika kabla kuadhimisha Alhamisi Takatifu kwa kuosha na kubusu miguu ya wafungwa kwenye gereza mjini Rome hii ikiwa ni mara ya kwanza kwa papa kufanya ibada hiyo gerezani na kwa mara ya kwanza kuwajumuisha wanawake na Waislamu.Papa Francis mwenye umri wa miaka 76 amesema katika misa kwenye gereza la vijana la Casal de Marmo ikiwa ni wiki mbili baada ya kuteuliwa kuwa papa wa kwanza kutoka Amerika Kusini kwamba yoyote yule alieko juu lazima ahahudumie wengine.Amesema anafanya hayo kwa moyo wake wote kwa sababu ni wajibu wake akiwa mchungaji na akiwa askofu na kwamba inabidi awahudumie watu.Msemaji wa Vatikan Federico Lombardi amesema washiriki wengi walibubujikwa na machozi katika ibada hiyo ambayo ilikuwa wazi kwa vyombo vya habari vya Vatikan tu.Ukanda wa video umeonyesha Papa akiimwagia maji miguu ya wafungwa hao 12 mmojawapo ukikwa na tatoo ambapo aliinama na kuibusu.

Papa Francis akijiandaa kuosha miguu ya wafungwa.
Papa Francis akijiandaa kuosha miguu ya wafungwa.Picha: Getty Images

Ibada ya Alhanmisi Takatifu

Lombardi amesema wakati hii ni mara ya kwanza kwa Papa kuosha miguu ya wanawake Francis aliwahi kufanya ibada ya aina hiyo katika nchi yake ya Argentina mara nyingi kabla ya kuwa papa kwenye magereza, hospitali na nyumba za kutunza wazee.Ibada ya siku ya Alhamisi Takatifu kwa kawaida hufanyika kanisani katikati ya mji na kuadhimisha ishara ya unyenyekevu inayoaminika kutekelezwa na Yesu Kristo kwa wafuasi wake 12 wakati wa chakula chao cha mwisho.Papa wanaofanya ibada hiyo kwa kawaida huwa wanaiosha miguu ya wachungaji.

Papa Francis akiosha mguu wa mfungwa gerezani katika Ibada ya Alhamisi Takatifu.
Papa Francis akiosha mguu wa mfungwa gerezani katika Ibada ya Alhamisi Takatifu.Picha: Reuters

Leo Papa atashiriki katika mkesha wa jioni ya Pasaka katika kanisa la Mtakatifu Peter na Jumapili papa huyo wa kwanza ambaye hatoki Ulaya kwa takriban miaka 1,300 atasheherekea misa ya Pasaka mbele ya maelfu ya mahujaji katika uwanja wa Kanisa la Mtakatifu Peter na baadae kutowa baraka zake za jadi za "Urbi et Orbi" kwa Rome na dunia kwa jumla.

Mwandishi: Mohamed Dahman/AFP

Mhariri: Hamidou,Oumilkher