Pendekezo la mkutano wa kimataifa wa amani ya mashariki ya kati.
24 Septemba 2007Mkutano huo uliwaleta pamoja katibu mkuu wa umoja wa mataifa Ban Ki Moon, waziri wa mambo ya nje wa marekani bi Condoleza Rice, waziri wa mambo ya nje wa urussi Sergei Lavrov, mwakilishi wa mambo ya nje wa umoja wa ulaya Javier Solana na aliyekuwa waziri mkuu wa zamani wa uingereza Tony Blair.
Wakati wa mkutano huo Bw Blair alitoa ripoti yake ya kwanza tangu alipoteuliwa mjumbe maalum wa mashariki ya kati mwezi juni mwaka huu.
Marekani imewashangaza wengi kwa kuialika Syria katika mkutano huo, uliopendekezwa na rais George Bush. Mkutano huo pia utahudhuriwa na wanachama wa jumuiya ya mataifa ya kiarabu na mashirika mengine kimataifa.
Wanchama hao ni pamoja na taifa la Jordan, Misri haya yakiwa mataifa mawili tu ya kiarabu yaliyotia saini mkataba wa amani na Israel.Mataifa mengine ni pamoja na qatar, umoja wa falme za kiarabu na saudi arabia.
Hata hivyo katika mkutano huo Bi Rice hakuitaja Syria miongoni mwa mataifa ya kiarbu yaliyoalikwa kwenye mkutano huo.Syria inashtumiwa kuhusika katika mauaji ya watu mashuhuri katika taifa jirani la Lebanon na pia kuruhusu kuingizwa kwa silaha na kuunga mkono wapiganaji nchini Iraq.
Pande hizo nne zinazounga mkono mashauri ya amani katika mashariki ya kati katika mkutano huo hazikuunga mkono waziwazi tangazo la hivi majuzi na israel la kulitaja eneo la
ukanda wa gaza kuwa hatari. Israel tayari imetishia kukatisha huduma zote muhimu katika eneo hilo linalosimamiwa na wapiganaji wa kundi la Hamas.
Hata hivyo walisema kuwa hali ni mbaya katika ukanda wa gaza na kusisitiza umuhimu wa kutolewa kwa msaada wa dharura.
Bw Blair pia alitangaza kufanyika kwa mkutano wa wafadhili kwa mamlaka ya palestina utakaofanywa baadaye mwaka huu. Katika mkutano huo watajidili njisi ya kutoa msaada wa kifedha kwa Palestina. Marekani na umoja wa ulaya zilisimamisha msaada kifedha wa moja kwa moja kwa palestina mwaka jana baada ya kundi la Hamas ambalo wanalitaja kama la kigaidi kushinda uchaguzi wa ubunge.