1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Putin aapishwa kuongoza Urusi

7 Mei 2012

Vladimir Putin ameapishwa kuwa rais wa Urusi akirudi Ikulu ya Kremlin baada ya kushika wadhifa wa uwaziri mkuu wa nchi hiyo kwa kipindi cha miaka minne, huku kukitokea maandamano makubwa kuupinga utawala wake.

https://p.dw.com/p/14r3G
Vladimir Putin speaks with his hand on the Constitution during his inauguration ceremony as new Russia's president in Moscow Monday, May 7, 2012. Putin has been sworn in as Russia's president for a third term after four years as prime minister. (AP Photo/RIA Novosti Kremlin, Vladimir Rodionov, Presidential Press Service)
Rais Vladimir PutinPicha: AP

Kwa mara ya kwanza kabisa rais Putin alichaguliwa kama rais wa Urusi mwaka 2000 na kwa awamu hii mpya ya miaka sita, itamweka madarakani mpaka mwaka 2018.

Hafla ya kuapishwa kwa kiongozi huyu imefanyika chini ya ulinzi mkali katika ukumbi wa St. Andrew uliopo katika Ikulu ya Kremlin. Kiasi cha maafisa waaandamizi 3000 wa serikali ya Urusi walihudhuria hafla hiyo.

Kiongozi wa kanisa la madhehebu ya Orthodox alimpa baraka zake Putin na maafisa wa jeshi wa taifa walimkabidhi mamlaka ya kusimamia kikosi cha nyuklia cha taifa hilo.

Akiwa ameshika katiba mkono wake wa kulia, Putin ameapa kuheshimu na kulinda haki na uhuru wa watu wa taifa lake. Katika hotuba yake fupi pia ameahidi kufanya jitiahada mpya katika kufanikisha kasi ya maendeleo.

Kiongozi huyo ameiita siku ya leo kuwa ya kihistoria kwa kuingia katika hatua mpya ya maendeleo kwa hivyo wanajukumu jipya la kufikia viwango vikubwa vya kimaendeleo.

Kuapishwa kwa Putrina kunafanyika ikiwa ni siku moja tu baada ya kufanya maandamano makubwa yaliojumuisha takribani watu 20,000 ambao ni pungufu ya wale walijitokeza hadharani muda mfupi baada ya uchaguzi wenyewe. Hata hivyo kiapo hicho pia kinafanyika wakati hasira za umma dhidi ya kiongozi huyo kurejea ikulu ya Kremlin hazijatoweka.

Russian riot police detain a participant during a "march of the million" opposition protest in central Moscow May 6, 2012. Thousands of people took to the streets of several Russian cities on Sunday to protest against Vladimir Putin on the eve of his return to the presidency, but opposition hopes of staging a "march of a million" fell flat. REUTERS/Denis Sinyakov (RUSSIA - Tags: POLITICS CIVIL UNREST)
Polisi wakikabiliana na WaandamanajiPicha: Reuters

Maandamano hayo ambapo waandamanaji walijaribu kukusanyika katika eneo la ikulu ya nchi hiyo yaligeuka kuwa vurugu pale ambapo polisi ilipofanya jaribio la kuwatawanya.

Polisi waliovalia mavazi ya kujikinga na vurugu walipiga umma huo kwa fimbo na kufanikiwa kuwaweka kizuizini zaidi ya watu 400.

Putin amehudumu mihula miwili kama rais wa Urusi kuanzia mwaka 2000 mpaka 2008 kabla hajaondoka na kuacha madaraka kwa Dmitry Medvedev kushikiliwa wadhifa huo kwa muhula mmoja kuanzia 2008 mpaka mwaka huu wa 2012.

Mabadiliko ya sasa katika katiba ya Urusi yanatoa ridhaa ya rais kuongoza kwa taifa hilo kutoka miaka minne mpaka sita. Na Rais Putin amekwisha sema ataweza kuwania nafasi hiyo ya urais kwa muhula mwingine wa nne kama ataungwa mkono na Warusi.

Hivi sasa wakosoaji wanamlalamikia Rais Putin kwa kuiweka rehani haki za raia wa nchi hiyo kufuatia uchaguzi ulimweka madarakani wa Machi 4 ambapo inadaiwa kufanyika ulaghai.

Mwandishi: Sudi Mnette/APE/AFP
Mhariri: Mohammed Khelef