1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Barack Obama apata nguvu mpya kufufua uchumi Marekani.

Eric Kalume Ponda29 Januari 2009

Juhudi za Rais wa Marekani Barack Obama kufufua uchumi wa taifa hilo leo zilipata nguvu mpya baada ya bunge la waakilishi kuuidhinisha mpango wa dola bilioni 819 kuokoa uchumi huo ulioporomoka.

https://p.dw.com/p/GiTU
Rais Barack Obama sasa kutumiza ndoto yake kufufua Uchumi.Picha: AP

Uchumi wa Marekani uliporomoka na kufika kiwango cha kutisha na kampuni nyingu kufungwa wakati wa utawala wa mtangulizi wake George W Bush.


Huu ni ushindi wa kwanza wa Rais Barack Obama kumwezesha kutimiza ahadi alizotoa wakati wa kampeini zake za kuunda nafasi zaidi za kazi na kuimarisha maisha ya raia wa Marekani kwa ujumla.


Mpango huo ambao kwa sasa unasubiri kuidhinishwa na bunge la Congress, umeidhinishwa na bunge la wakilishi kwa kura 244 dhidi ya 188, huku wabunge 11 wa chama cha Democrats cha Rais Barack Obama wakiungana na wale wa Republican kuupinga mpango huo.


Rais Barak Obama alisema kuwa hii ni hatua muhimu na yuko tayari kufanya marekebisho yanayostahiki kabla ya kuwasilishwa kwa baraza la Senate. Rais Barak Obama anasema kuwa anatarajia kutia saini mpango huo na kuwa sheria kabla ya mwezi ujao kumalizika.


Akisema kuwa mpango huo utaweza kuimarisha huduma na bima za afya na makaazi bora kwa raia wengi wa Marekani, Rais Obama alisisitiza kuwa huu si wakati wa bunge la Marekani kujikokota katika kuokoa uchumi wa taifa hilo.

Rais Obama alisema ``Wafanyi kazi wanaorejea nyumbani kuwambia wake zao waume zao na watoto kwamba sasa hawana tena kazi, na wale wanaphofia kuppoteza kazi katika siku za hivi punde wanahitaji kusaidiwa hivi sasa. Wanatarajia kuona suala hili likishughulikiwa na Washington kwa haraka. Na ndio sababu nataraji kutia saini mpango huu katika muda wa wiki chache zijazo´´.


Wakiidhinisha mpango huo uliozua utata,wabunge hao walisema kuwa wanataka kuona miradi yote inayotekelezwa chini ya mpango huo ikitumia malighafi kutoka nchini humo hasa vyuma.


Iwapo mpango huo utaidhinishwa , utawala wa Rais Barack Obama unakusudia kutumia kiasi cha dola bilioni 358 kuanzisha miradi ya ujenzi na kupanua shughuli za uekezaji ili kubuni nafasi zaidi za ajira.


Kitita cha dola bilioni 275 kitatumiwa kupunguza kwa muda kodi ya mapato kwa wafanyi kazi, kutoa motisha kwa kampuni za ujenzi na viwanda ili ziweze kutoa nishati inayoweza kutumia tena na tena, na kuzisaidia kampuni kufidia hasara zilizopata katika muda wa miaka mitano iliyopita.


Kadhalika kiasi kingine cha Dola bilioni 48 kitatumiwa kuzisaidia familia bima zao za afya na teknolojia yahabari kuhusu afya.


Chama cha Republican hakikuwa na idadi ya kutosha kupinga mpango huo ingawa kuna hofu kwamba huenda wakafanya hivyo punde tu utakapowasilishwa kwa baraza la Senate ambako wanaidadi ya kutosha kuupinga iwapo watafanikiwa kuwashawishi wabunge wachache wa chama cha Democrats.


Spika wa bunge Nancy Pelosi ambaye ni kutoka chama cha Democrats alitaja hatua hiyo kuwa ushindi wa Marekani akisema kuwa utawezesha kuundwa nafasi za ajira kati milioni 3 na 4 nchini humo.


Hatua hiyo imetokea wakati ambapo ripoti ya shirika la fedha Duniani inakadiria kuwa uchumi wa Marekani utashuka kwa kiwango cha mwaka huu wa 2009.


Ponda/Afp-Reuters