1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Obama mbioni kuunda timu yake.

Mtullya, Abdu Said6 Novemba 2008

Rais mteule wa Marekani yumo katika juhudi za kuunda timu itakayomsaidia kuongoza.

https://p.dw.com/p/FoSx
Rais mteule Barack Obama katika juhudi za kuunda timu ya kumsaidia kuongoza.Picha: AP

Rais Mteule wa Marekani Barack Obama ameweka kando sherehe za ushindi wake ili kuanza kuunda timu itakayomsaidia kuiongoza nchi ambayo sasa inakabiliwa na mgogoro wa uchumi sambamba na vita vya nchini Irak na Afghanistan.

Ni muda mfupi tokea Barack Obama atangazwe mshindi wa uchaguzi wa rais nchini Marekani lakini ameshaanza kuchukua hatua za kuwaleta pamoja watu watakaomsaidia kurithi nchi inayokabiliwa na mgogoro mkubwa wa fedha usiokuwa na mithili katika historia ya hivi karibuni nchini Marekani.

Obama ataingia Ikulu wakati ambapo Marekani inapigana vita nchini Irak na Afghanistan.Habari kutoka Chicago zinasema rais mteule Barack Obama anafirikia kumteua Rahm Emanuel kutoka Illinois kuwa mnadhimu mkuu wake. Rahm Emanuel ambaye kwa sasa ni mbunge aliwahi kuwa mshauri wa rais Bill Clinton.

Mbunge huyo mwenye umri wa miaka 48 ana uhusiano wa ndani na wapambe wa Obama na yeye pia anatoka Chicago.

Habari zaidi zinasema rais mtuele Obama huenda leo akamtangaza waziri wa fedha -mtu anaemhitaji sana katika kukabiliana na mgogoro mkubwa wa fedha.

Obama tayari ameshazindua timu ya mpito inayoharakisha kazi ya kuwatafuta watu watakaoshughulikia masuala ya usalama na uchumi.

Katika mazingira ya mgogoro mkubwa wa fedha usiokuwa mithili tokea kuanguka kwa uchumi wa dunia mnamo mwaka 1929 Obama anakusudia kuchukua hatua za haraka ili kuwa tayari kukabiliana na tishio la kudorora kwa uchumi na kushughulikia vita vya Irak na Afghanistan.Obama amesema changamoto kubwa zinaisubiri zinaikabili Marekani.

Wadadisi wa sera za nje wanasema rais mteule Obama atakabiliwa na kazi kubwa katika kujaribu kurejesha wajihi mzuri wa Marekani nchi za nje uliovurugwa na utawala wa Bush.

Jukumu hilo huenda likaenda kwa John Kerry ,seneta wa Massachusetts aliewahi kugombea urais dhidi ya G. Bush. Hatahivyo majina mengine pia yametajwa ikiwa pamoja na la mwanadiplomasia wa siku nyingi, Richard Holbrooke .

Habari zaidi zinasema, kwa kuwa vita vya nchini Irak na Afghanistan bado vinaendelea, huenda Obama akambakiza waziri wa ulinzi wa sasa Robert Gates.

Wakati huo huo rais G.W Bush ameahidi kushirikiana na rais mteule Obama katika kipindi cha mpito hadi hapo bwana Obama atakapoingia madarakani rasmi tarehe 20 mwezi januari. Mkuregenzi wa shirika la ujasus CIA, Mike Hayden pia ameahidi kushirikiana na rais mteule Obama.