1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Obama atetea msimamo wake

Oumilkher Hamidou22 Mei 2009

Purukushani hazishi kuhusu mpango wa kufungwa Guantanamo

https://p.dw.com/p/HvDo
Rais wa Marekani Barack ObamaPicha: dpa

Rais Barack Obama,akitoa hotuba muhimu kuhusu usalama wa taifa, amesisitiza dhamiri zake za kuifunga kambi ya wafungwa ya Guantanamo na kutetea fikra ya kuhamishiwa baadhi ya wafungwa katika jela za Marekani,licha ya mabishano makali yaliyoripuka.

Rais Barack Obama amejaribu kutuliza hofu zinazotokana na uamuzi wake wa kuifunga kambi ya wafungwa ya Guantanamo hadi january mwaka 2010,huku akitetea kikamilifu msimamo wake dhidi ya hujuma toka mrengo wa kulia na mrengo wa shoto dhidi ya siasa yake ya usalama wa taifa.

Matamshi yake hayajaonyesha kutuliza mvutano unaotokana na mwito wa rais wa kufufua uchumi na kuifanyia marekebisho sekta ya huduma za jamii.Mashirika yanayotetea uhuru bado yanaendelea kulalamika.Kwa upande wa mrengo wa kulia ,makamo wa zamani wa rais Dick Cheney amemtuhumu rais Obama kuutia hatarini usalama wa wamarekani.Na wabunge wanaodai wapatiwe mpango timamu wa kufungwa kambi ya wafungwa ya Guantanamo,na wao pia hawajaridhika.

Ghasia zilizozushwa na hoja za kutaka kuachana na mitindo ya enzi za Bush zimezidi hivi sasa baada ya hata marafiki wa rais Obama wa chama cha Democratic katika baraza la Senet,kuungana na warepublican,angalao kwasasa na kukataa kumkubalia dala milioni 80 zinazohitajika kuweze kukamilisha mipango ya kuifunga kambi ya wafungwa ya Guantanamo.Wanahofia watuhumiwa wa kigaidi wasije wakasalia nchini Marekani,katika jela au majiani na wanataka kujua kwa undani zaidi Obama anapanga kuwafanya nini wafungwa 240.

Rais Obama anawajibu akisema:

"Badala ya kutufanya tuishi salama,kambi ya wafungwa ya Guantanamo imedhoofisha usalama wa Marekani.Inatumiwa na maadui zetu kuzidi kutukosoa,inapunguza azma za washirika wetu kushirikiana nasisi katika kupambana na adui.Lakini kwa vyovyote vile gharama za kuifanya iendelee kuwa wazi ni kubwa kuliko zile za kuifunga.Ndio maana katika kampeni yangu ya uchaguzi nimepigania ifungwe na ndio maana nnataka ifungwe mwaka mmoja kutoka sasa."

"Kampi ya wafungwa ya Guantanamo imechafua maadili ya Marekani ulimwenguni na kuwepo kwake kumezidisha magaidi kuliko wale wanaoshikiliwa." amesema rais Obama aliyeikosoa serikali iliyotangulia.

Amekumbusha dhamniri zake za kuachiwa wafungwa watakaotakaswa na mahakama ,kufikishwa katika mahakama za kiraia idadi kubwa zaidi ya watuhumiwa wengine na kama haiwezekani wafikishwe mbele ya mahakama za kijeshi, na wengine wapelekwe katika nchi zitakazokubali kuwapokea.

Amekiri kuna wafungwa ambao hawawezi kuachiliwa huru au kuhamishiwa ng'ambo na kwamba watuhumiwa hao wanaendelea kutishia usalama.Hata hivyo anasema wanaweza kushikiliwa kwa muda usiojulikana mwisho.

Georgien USA Vizepräsident Dick Cheney bei Michail Saakaschwili in Tiflis
Makamo wa´zamani wa rais Dick CheneyPicha: AP

Licha ya hotuba hiyo,rais Obama anakosolewa na kila upande.Makamo wa zamani wa rais Dich Cheney anasema tunanukuu:"Nahisi baada ya kutafakari,rais atatambua hatari kubwa inayoweza kutokea ikiwa magaidi wataachiwa waingie nchini."Mwisho wa kumnukuu.

John Boehner wa chama cha Republican amemtaka rais Obama awaonyeshe mpango wake uko wapi wa kuifunga kambi ya Guantanamo?

Hata mkuu wa kundi la Democratic katika baraza la Senet Harry Reid amesema bado anausubiri mpango huo.

Hata mashirika yanayopigania haki za binaadam hayajaridhika.

Human Rights watch linasema kuendelea kuwashikilia wafungwa bila ya kuwafikisha mahakamani ni sawa na kufanya maovu yale yale yaliyofanywa na utawala wa Bush.

Na shirika la Amnesty International linakosoa vikali kuendelea kuwepo mahakama za kiijeshi.

Mwandishi : Ommilkheir Hamidou /AFPE

Mhariri:Abdul-Rahman