1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Obama kukutana na rais wa Palestina Mahmoud Abbas.

Sekione Kitojo27 Mei 2009

Wapalestina wana shaka iwapo mkutano kati ya rais Mahmoud Abbas na Barack Obama utaleta mbinyo kwa Israel kubadili msimamo wake dhidi ya Palestina.

https://p.dw.com/p/HyX3
Rais Barack Obama akipunga mkono wakati akishuka kutoka katika ndege ya Air Force 1. Atakutana na rais wa Palestina Mahmoud Abbas siku ya Alhamis.Picha: AP


Wapalestina wameeleza shaka shaka yao leo

Jumatano kuwa ziara mjini Washington ya rais Mahmoud Abbas , na mkutano wake na rais wa Marekani Barack Obama siku ya Alhamis unaweza kusababisha mbinyo kwa Israel kuondoka kutoka katika maeneo inayoyakalia.


Kwa mujibu wa mwandishi wa makala maalum, Omar Ghoul , akiandikia katika gazeti linaloelemea upande wa rais Abbas la al-Hayat al-Jadida, tatizo la Abbas na utawala wa rais Obama ni kwamba Obama anafuata sera za Israel za mkwamo, na anachukua mtazamo wa tahadhari kuhusiana na ubabe wa Israel dhidi ya watu wa Palestina.

Utawala wa Marekani , amesema unapatana na Israel katika masuala muhimu kwa Wapalestina, kama haki ya wakimbizi wa Kipalestina na vizazi vilivyopo hivi sasa kurejea katika makaazi yao waliyoyakimbia mwaka 1948 hadi 49 katika vita kati ya Israel na Waarabu , suala la Jerusalem mipaka pamoja na makaazi ya walowezi wa Kiyahudi.

Hali hii inamfanya rais Abu Mazen au Abbas, na uongozi wa Palestina kuwa katika shaka ya kupatikana njia kuelekea maelewano katika sera za Marekani, kuelekea mzozo kati ya Israel na Palestina, amesema Ghoul.

Abbas ameeleza matumaini yake katika mji mkuu wa Canada, Ottawa, ambao ameutembelea kabla ya kwenda Washington jana Jumanne usiku, kuwa utawala wa rais Obama utailazimisha Israel kusitisha ujenzi wa makaazi yote ya walowezi wa Kiyahudi katika ukingo wa magharibi na kukubali suluhisho la kuwa na mataifa mawili.

Amesema kuwa mazungumzo ya amani hayataanza kabla ya Israel kukubali suluhisho la kuwa na mataifa mawili na kuacha kupanua makaazi ya walowezi wa kiyahudi . Mpango wowote wa amani ni lazima uelekeze kufikisha mwisho kwa hatua ya Israel kuikalia Palestina, iliyoanza mwaka 1997 na kuundwa kwa taifa la Palestina litakalokuwapo sambamba na taifa la Israel.

Msemaji wa rais Abbas , Nabil Abu Rudeineh, ambaye anasafiri na Abbas , pia amesema katika taarifa kwa vyombo vya habari kuwa rais wa Palestina atamfahamisha rais wa Marekani kuwa Wapalestina hawataki kusikia maneno, lakini wanataka kuona vitendo.

Waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu , ambaye alikutana na rais Obama Mei 18, amekataa kuidhinisha suluhisho kwa ajili ya mzozo huo ambalo litasababisha kuwapo taifa la Israel na Palestina yakiishi kwa pamoja.

Amesema kuwa baada ya Abbas kukutana na Obama , tutaweza kutoa uamuzi kuwa tukitarajia msimamo wa Marekani ni kupoteza wakati kwasababu hakuna kitu cha kutufanya tuamini kuwa kuna kitu kipya kuelekea upande wa Wapalestina na Marekani haitaiwekea mbinyo Israel ama kudai kutoka utawala wa nchi hiyo kubadilisha sera zake kuelekea Palestina.

Wakati huo huo waziri wa mambo ya kigeni wa Uingereza David Milliband leo amehimiza kuwapo na juhudi kubwa kufufua hatua za kuleta amani katika mashariki ya kati, akionya kuwa mkwamo uliopo hivi sasa utasababisha ugumu wa kufikia suluhisho.


Mwandishi Sekione Kitojo / DPAE

Mhariri Othman , Miraji

►◄