1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ziara ya kwanza ya kiongozi magharibi tangu 2004

7 Septemba 2015

Rais wa Austria Heinz Fischer anatarajiwa kuanza ziara nchini Iran na hivyo kuwa mkuu wa kwanza wa nchi ya Magharibi kufanya ziara katika nchi hiyo baada ya kutiwa saini mkataba wa nyuklia

https://p.dw.com/p/1GS5F
Austria mwenyeji wa mazungumzo juu ya mpango wa nyuklia wa Iran
Austria mwenyeji wa mazungumzo juu ya mpango wa nyuklia wa IranPicha: Reuters/L. Foeger

Rais huyo wa Austria anaenza ziara ya siku tatu nchini Iran leo ni kiongozi wa kwanza wa nchi ya magharibi kwenda katika nchi hiyo tokea mwaka wa 2004 . Rais wa Austria wa wakati huo Thomas Klestil alikuwa kiongozi wa mwisho wa nchi ya magharibi kufanya ziara nchini Iran.

Katika ziara yake Rais Henz Fischer atakutana na Rais wa Iran Hassan Rouhani na Waziri wa mambo ya nje wa Mohammad Javad Zarif. Rais wa Austria pia atakutana na Kiongozi mkuu wa Iran Ayatollah Ali Khamenei, kadhia inayozingatiwa kuwa ya nadra kwa sababu Rais Heinz Fischer siyo kiongozi anaetoka katika nchi ya kiislamu.

Kabla ya kuondoka Rais wa Austria alisema kuwa kwenye mazungumzo na wenyeji wake wa Iran atayazingatia masuala ya haki za binadamu vile vile

Haki za binadamu zitajadiliwa

Umoja wa Mataifa ulisema, mnamo mwezi wa Machi ,katika ripoti yake inayotolewa kila mwaka kwamba hali ya haki za binadamu nchini Iran inasumbua kutokana na idadi kubwa ya watu walionyongwa mnamo mwaka uliopita. Inaaminika kwamba watu zaidi ya 500 walinyongwa nchini Iran kati ya mwezi Januari na mwezi Novemba mwaka uliopita. Lakini Iran imeyakanusha madai hayo.

Pamoja na masuala ya kibiashara Rais wa Austria pia atalijadili suala la wakimbizi na wenyeji wake. Hapo awali aliisiitiza umuhimu wa kuing'oa mizizi ya mgogoro wa wakimbizi. Amesema jambo la kipaumbele na njia ya ufanisi mkubwa kabisa ni kuweka mkazo wote katika kuzuia na kuvikomesha vita vya nchini Syria vinavyosababisha maalfu ya wakimbizi".

Kwa upande wake Iran inawaona magaidi wanaoitwa dola la kiislamu kuwa chanzo cha idadi kubwa ya wakimbizi wanaomiminika katika nchi za Ulaya.

Sawa na nchi nyingine nyingi za Umoja wa Ulaya Austria pia inataka kuanzisha zama mpya za uhusiano na Iran. Katika kipindi cha miaka mitano ijayo Austria na Iran zinapanga kuongeza kiwango cha biashara baina yao mara tano. Kwa sasa nchi hizo zinafanya biashara thamani ya Euro Milioni 232.

Austria ambayo haikuvunja uhusiano wake na Iran baada ya mapinduzi ya mwaka wa 1979, ilikuwa mwenyeji wa mazungumzo marefu yaliyouleta mkataba wa nyuklia, uliotiwa saini baina ya Iran na mataifa makubwa duniani.

Mwandishi:Mtullya abdu/dpa,afp,

Mhariri:Josephat Charo