1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mgogoro bado upo!

Abdu Said Mtullya4 Septemba 2009

Rais wa benki Kuu ya Ulaya Jean-Claude Trichet amesema mgogoro wa uchumi bado haujamalizika.

https://p.dw.com/p/JSV3
Rais wa benki Kuu ya Ulaya Jean-Claude Trichet.Picha: AP

Rais wa Benki kuu ya Ulaya, Jean Claude Trichet, amesema  kuwa mgogoro wa fedha ulioikumba dunia bado haujamalizika kabisa.

 Bwana Trichet amesema hayo  leo  mjini Frankfurt baada  ya  tamko la benki la hapo jana kuwa  uchumi unaanza kuinuka tena.

Akizungumza baada ya benki  Kuu  ya Ulaya kuendeleza riba katika kiwango cha kihistoria cha  asilimia moja,  bwana Trichet amesema leo kuwa  mgogoro wa fedha  bado ungalipo na kwamba benki   kuu  ya  Ulaya itaendelea kuchukua hatua za kuyaunga mkono mabenki kwa kadri itakavyowezekana.

Wachunguzi wanasema  rais huyo  wa benki amesema hayo  leo  kusahihisha tamko la benki yake la  hapo jana  la  kuonesha matumaini juu  ya  kumalizika   kwa mgogoro wa  uchumi.

Lakini rais huyo  wa benki Kuu ya Ulaya ameeleza   kuwa  ni mapema mno kusema mgogoro  wa  fedha umemalizika.

Bwana Trichet alikuwa anazungumza na wataalamu kwenye kongamano lililoandaliwa na taasisi  ya mitaala ya  fedha  kwenye chuo kikuu cha Göthe cha mjini Frankfurt.

Hatahivyo, bwana Trichet  ameeleza wazi kwamba  mabenki  hatimaye  yatapaswa kusimama yenyewe tena  kwa migumu yao .

Rais  huyo wa benki kuu ya  Ulaya  pia alifafanua  juu ya mkakati  wa  kuanza kufunga  breki katika hatua  za benki  ambazo zimekuwa  zinachukuliwa  katika kipindi cha miaka 2 iliyopita.

Benki  kuu ya Ulaya imepunguza  riba  kutoka asilimia 4.25 na imetoa mikopo mikubwa  kwa mabenki katika kipindi cha zaidi  ya mwaka mmoja.

Hatahivyo,  bwana Trichet amesema benki yake itaacha  kutekeleza hatua za kuyasaidia mabenki  ikiwa uchumi  utarejea  katika  hali ya kawaida.

Hatua zilizochukuliwa  na benki ya  Ulaya katika kutoa mikopo  zilizisaidia  nchi za Ulaya  katika kukabiliana na mgogoro  wa uchumi, lakini licha  ya hatua hizo nchi 16 zinazotumia  sarafu ya Euro  ziliingia  katika mdodoro  wa uchumi kwa mara ya  kwanza tokea mwaka  1999.

Baada ya kudorora kwa asilimia 0.1 katika robo ya pili mnamo mwaka huu, eneo la nchi zinazotumia  sarafu  ya Euro lipo njiani kuelekea kwenye ustawi.

Akisisitiza  matumaini hayo, mkuregenzi wa shirika la fedha la kimataifa, IMF, Dominique Strauss -Kahn, amesema leo mjini Berlin kwamba  uchumi  wa  dunia   unaanza kuinuka  tena na kwamba nchi sasa zinapaswa kupanga namna ya  kuacha kutekeleza hatua za kufufua  uchumi.

Mwandishi/Mtullya  Abdu/AFPE.

Mhariri/. Miraji Othman