1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais wa Ujerumani Christian Wulff ajiuzulu

Abdu Said Mtullya17 Februari 2012

Rais wa Ujerumani Christian Wulff amejiuzulu baada ya kuutumikia wadhifa huo kwa muda wa siku 598.Bwana Wulff amechukua hatua hiyo kutokana na shinikizo la Mwendesha Mashtaka Mkuu wa serikali

https://p.dw.com/p/1452I
Rais wa Ujerumani Christian Wulff(Kulia)
Rais wa Ujerumani Christian Wulff(Kulia)Picha: picture-alliance/dpa

Hatua hiyo inatokana na uamuzi wa mwendesha mashtaka Mkuu wa serikali kukusudia kuzichunguza tuhuma za rushwa zinazomkabili bwana Wulff. Akieleza sababu ya kujizulu, Bwana Wulff alisema haukuwezekana kwake kuendelea kufanya kazi kwa kadri ilivyohitajika.

Katika tamko lake la kujiuzulu bwana Wulff alisema ,Ujerumani inamhitaji Rais anaeweza kuyatekeleza majukumu makubwa yote ya ndani na ya nje bila ya vipingamizi . Pia amesema Ujerumani inamhitaji Rais mwenye imani ya idadi kubwa ya watu wake. Lakini amaeleza kuwa matukio ya hivi karibuni yaliathiri utendaji kazi wake.

Bwana Wulff amesema matukio ya siku na wiki za hivi karibuni yameonyesha, kwamba uwezo wake wa kutenda kazi uliathirika.Kutokana na sababu hiyo, haikuwezekana kwake kuyatekeleza majukumu ya ofisi ya Rais ya ndani na ya nje, kama jinsi inavyopasa. Lakini Wulff alikiri kutenda makosa.Hata hivyo amesema alikuwa mkweli.

Wulff ameeleza kuwa taarifa za vyombo vya habari juu yake katika miezi miwili iliyopita zilimwathiri yeye pamoja na mke wake. Wulff alieutumikia wadhifa wa urais kwa muda wa siku karibu 600 amezikanusha tuhuma zote zilizotolewa juu ya yake. Mwanasiasa huyo mwenye umri wa miaka 52 amesema ameamua kuondoka kwa sababu hakuweza tena kufanya kazi zake kama jinsi ambavyo ingehitajika.Amesema amechukua hatua hiyo kutokana na kupoteza imani miongoni mwa wananchi

Kansela wa Ujerumani Angela Merkel katika tamko lake juu ya kujiuzulu kwa Bwana Wulff alimsifu kwa kuchukua hatua sahihi. Lakini wakati huo huo Merkel amearifu kwamba anakusudia kukukutana na viongozi wa vyama vya upinzani ili kuanza mazungumzo ya kumtafuta mtu atakaechukua nafasi ya Bwana Wulff ambae atakubalika na wote.

Christian Wulff ni Rais mwengine aliejiuzulu mnamo kipindi cha miaka miwili. Rais wa hapo awali Bwana Horst Köhler alijiuzulu ghafla mnamo mwezi wa mei mwaka 2010 , baada ya kutoa kauli juu ya jukumu la jeshi la Ujerumani nchini Afghanistan.

Mwandishi/Stützle Peter
Tafsiri/Mtullya Abdu
Mhariri/Abdul-Rahman