1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ribery aurefusha mkataba wake Bayern

7 Juni 2013

Mshambuliaji wa Ufaransa Franck Ribery amesaini mkataba wa miaka miwili na Bayern Munich, hadi mwaka wa 2017. Beki Mbelgiji Daniel van Buyten pia ameongeza mwaka mmoja kwenye mkataba wake hadi mwishoni mwa msimu

https://p.dw.com/p/18lrI
Bayern Munich's Franck Ribery celebrates after a goal was scored against Barcelona during their Champions League semi-final second leg soccer match at Camp Nou stadium in Barcelona May 1, 2013. REUTERS/Albert Gea (SPAIN - Tags: SPORT SOCCER)
Champions League 2013 Halbfinal Rückspiel FC Barcelona FC Bayern MünchenPicha: Reuters

Wakati huo huo beki wa Borussia Dortmund raia wa Poland Lukasz Piszczek anatarajiwa kuwa mkekani kwa miezi mitano baada ya kufanyiwa upasuaji wa nyonga. Piszczek ni mmoja wa wachezaji muhimu wa Dortmund na aliisaidia kufika katika fainali ya Champions League, ambapo walishindwa mabao mawili kwa moja na Bayern Munich.

Jeraha la Mpoland huyo ni pigo kubwa kwa Dortmund, ambao pia walimpoteza kiungo mwenye kipaji Mario Götze aliyehamia Bayern Munich na beki Felipe Santana aliyejiunga na Schalke, naye mshambuliaji Robert Lewandowski akionekana kuhamia Bayern.

Lukasz Piszczek alikuwa kiongo muhimu katika safari ya Borussia Dortmund barani Ulaya
Lukasz Piszczek alikuwa kiongo muhimu katika safari ya Borussia Dortmund barani UlayaPicha: picture-alliance/dpa

Kwingineko, biashara ya kuwasajili wachezaji wapya inaendelea huku timu zikilenga kujiimarisha kabla ya msimu mpya kuanza. Huko England, mashabiki wa Arsenal angalau wanaweza kuwa na sababu ya kutabasamu, baada ya Afisa Mkuu Mtendaji wa timu hiyo Ivan Gazidis kusema kuwa hatimaye watatumia kiasi kikubwa kumwezesha kocha Arsene Wenger kuwanunua wachezaji nyota.

Hayo yanajiri wakati Manchester City ikiendelea kuiongeza nguvu kikosi chake, kwa kumsajili nyota wa Brazil, Fernandinho kutoka klabu ya Shakhtar Donetsk ya Ukraine kwa kiasi cha pauni milioni 35. Pia wamemsaini mshambulizi wa klabu ya Uhispania, Sevilla, Jesus Navas.

Wagombea sita wa IOC

Na wagombea sita wa kiume wanashiriki katika kinyang'anyiro cha kumrithi Jaque Rogge kama rais wa Kamati ya Kimataifa ya Olimpiki – IOC. Watu hao sita ni pamoja na – Mjerumani Thomas Bach, Sergey Bubka wa Ukraine, Mmarekani Richard Carrion, Ser Miang Ng wa Singapore, Denis Oswald kutoka Uswisi na Ching-Kuo Wu wa Taiwan. Wagombea hao walitangaza nia yao rasmi kabla ya muda wa mwisho wa Juni 6. Watawasilisha mipango yao, katika kikao cha faragha cha IOC mjini Lausanne mnamo Julai 3 na 4 mwaka huu.

Mjerumani Thomas Bach ni miongoni mwa wagombea sita wanaopigania nafasi ya kumrithi Jacque Rogge
Mjerumani Thomas Bach ni miongoni mwa wagombea sita wanaopigania nafasi ya kumrithi Jacque RoggePicha: picture-alliance/dpa

Timu zajiondoa CECAFA

Kinyang'anyiro cha kombe la vilabu vya Afrika Mashariki na Kati - CECAFA, ambacho kinatarajiwa kung'oa nanga tarehe 18 mwezi huu wa Juni hadi Julai 2, katika jimbo la Darfur, kinakabiliwa na hali ya sintofahamu. Vilabu vinaendelea kujiondoa vitikitaja sababu za kiusalama. Vilabu vya Tanzania Simba na Yanga vimetishia kujiondoa baada ya Waziri wa Mambo ya nchi za nje Benard Membe kusema bungeni kuwa hali ya usalama katika eneo hilo ni ya kutilia shaka.

Klabu ya Tusker ya Kenya pia imetangaza kujiondoa katika dimba hilo. Mwenyekiti James Musyoki amesema hawataki kucheza mechi zao katika mji wa Kadugli ambako wamepangwa kukaa wakati wa kinyang'anyiro hicho cha wiki mbili. Amesema hawataki kuyaweka hatarini maisha ya wachezaji wao pamoja na maafisa kutokana na kitisho cha usalama katika eneo hilo. Musyoki amesema watazingatia kushiriki katika dimba hilo kama litahamishwa sehemu nyingine.

Kujiondoa kwa vilabu hivyo viwili vya Tanzania, na kimoja cbha cha Kenya ni pigo kubwa kwa uhalali wa kinyang'anyiro hicho kufuatia maamuzi ya vilabu viwili vikuu nchini Sudan Al Hilal na Al Merreikh ya kutoshiriki. Mabingwa wa Ethiopia St George pia waliamua kutoshiriki katika dimba hilo ili kuendelea na kampeni yao ya Kombe la Shirikisho. Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Afrika Mashariki na Kati - CECAFA Nicholas Musonye amesisitiza kuwa dimba litaendelea jinsi lilivyopangwa awali, kwa sababu hali ya usalama katika eneo hilo ni shwari.

Mwandishi: Bruce Amani/DPA/AFP

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman