1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

RIYADH: Rais wa Sudan uso kwa uso na Ban Ki-Moon

27 Machi 2007
https://p.dw.com/p/CCF5

Rais Omar Hassan Al Bashir wa Sudana leo hii anatarajiwa kuwa na mazungumzo na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon, juu ya mzozo wa Darfur.

Rais huyo wa Sudan amekuwa akikataa juhudi za Umoja wa Mataifa kupeleka jeshi la kulinda amani la Umoja huo huko Darfur na pia kuwakabidhi watuhumiwa wa uhalifu wa kivita katika mahakama ya kimataifa ya uhalifu.

Maafisa wa Umoja wa nchi za Kiarabu wamesema kuwa mazungumzo hayo pia yanatarajiwa kuhudhuriwa na mfalme Abdullah wa Saudi Arabia, Mkuu wa Umoja wa Nchi za Kiarabu,Amr Mussa pamoja na mkuu wa Umoja wa Afrika, Alpha Konare.

Hapo jana Rais Bashir alikataa ombi la mahakama ya kimataifa ya uhalifu kumkabidhi waziri wa masuala ya kibinaadam wa Sudan Ahmed Haroun, kutokana na kutuhumiwa na mahakama hiyo kuhusika na uhalifu wa kivita.

Mwezi uliyopita mwendesha mashtaka wa mahakama hiyo, Luis Moreno Ocampo alimtuhumu Haroun pamoja na kiongozi wa kundi la wanamgambo wa Janjawidi kwa kuhusika na uhalifu wa kivita .

Wakati huo huo Umoja wa Ulaya umesema kuwa kutokuwepo kwa njia za kijeshi pamoja na uungaji mkono wa China katika Umoja wa Mataifa, umefanya ugumu katika utatuzi wa mzozo wa Darfur.

Waziri Mkuu wa Uingereza, Tonny Blair na Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel wameelezea umuhimu wa vikwazo zaidi dhidi ya Serikali ya Sudan.