1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Sanchez aitaka Arsenal kuamua hatima yake

Bruce Amani
17 Julai 2017

Mashabiki wa Arsenal wanasubiri kwa hamu kujua hatima ya mchezaji wao nyota Alexis Sanchez ambaye haijajulikana kama ataondoka msimu huu au la.

https://p.dw.com/p/2gg1r
Großbritanien Arsenal London vs FC Bayern München
Picha: Reuters/H. McKay Livepic

 Sanchez, ambaye ndiye alikuwa mfungaji bora wa Arsenal msimu uliopita akiwa na mabao 24 ya ligi kwenye mechi 38, anaingia mwaka wake wa mwisho katika mkataba wake na hajaweka saini mpya. Nyota huyo aliviabia vyombo vya habari mwishoni mwa wiki nyumbani kwao Chile kuwa anataka kucheza katika Ligi ya Mabingwa Ulaya na kuwa uamuzi wa mustakabali wake uko mikononi mwa waajiri wake "wazo langu ni kucheza champions league na kushinda taji hilo. ni ndoto niliyokuwa nayo tangu utotoni. ukweli ni kuwa uamuzi wa kuondoka Arsenal haunihusu mimi hasa. nimefanya uamuzi wangu. lakini sasa tusubiri kuona jibu la Arsenal, kwa kuzingatia wanachotaka".

Arsenal haikufuzu katika Champions League msimu uliopita baada ya kumaliza katika nafasi ya tano kwenye Premier League. Anahusishwa na vilabu vya Manchester City, Paris Saint Germain. Kiongozi Wa Bayern Karl Heinz Rummenigge amethibitisha kuwa klabu hiyo imeondoa nia yake ya kumsaini mshambuliaji huyo.

Arsenal wako China na watacheza dhidi ya mabingwa wa Ujerumani Bayern Munich siku ya Jumatano kabla ya kukwaruzana na mabingwa wa Premier League Chelsea siku ya Jumamosi.

Mwandishi: Bruce Amani
Mhariri: Yusuf Saumu