1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

SANTIAGO : Dikteta wa zamani Pinochet hatopewa maziko rasmi

11 Desemba 2006
https://p.dw.com/p/CCkN

Dikteta wa zamani wa Chile,Augusto Pinochet aliefariki siku ya Jumapili akiwa na umri wa miaka 91,hatopewa maziko rasmi na hakutotangazwa siku ya msiba nchini humo.Msemaji wa serikali aliarifu kuwa Pinochet atazikwa kwa heshima za kijeshi siku ya Jumanne mjini Santiago.Katika mwaka 1973 Pinochet,kwa msaada wa Marekani alimpindua rais wa Chile wa wakati huo,Salvador Allende aliechaguliwa kidemokrasia.Kiasi ya watu 3,200 ama waliuawa au walipotea wakati wa utawala wake wa kijeshi,kati ya mwaka 1973 na 1990.Kwa mujibu wa ripoti rasmi za Chile,kama wapinzani 30,000 wa dikteta huyo wa zamani walitiwa jela na kuteswa.Vile vile kiasi ya Wachile 20,000 waliikimbia nchi kwenda kuishi uhamishoni. Miongoni mwao,ni rais wa hivi sasa wa Chile Michelle Bachelet.Ingawa alishtakiwa kukiuka haki za binadamu na kufanya udanganyifu,Pinochet hajawahi kufikishwa mahakamani kwa sababu ya afya mbaya.