1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Schalke yaiangamiza Hamburg

Bruce Amani
20 Novemba 2017

Schalke imepanda hadi nafasi ya pili katika msimamo wa ligi kuu ya kandanda ya Ujerumani - Bundesliga baada ya kupata ushindi wa wa mabao mawili kwa bila dhidi ya SV Hamburg

https://p.dw.com/p/2nwob
Deutschland Bundesliga Schlake 04 gegen Hamburger SV | Burgstaller
Picha: Getty Images/AFP/P. Stollarz

Ushindi huo una maana kuwa Schalke wana pointi 23 sawa na RB Leipzig lakini schalke wana faida ya mabao. Max Meyer ni kiungo wa Schalke. "Tunafahamu kuwa inahusu kucheza kama kundi, kama tulivyocheza leo. Tulicheza kwa kulinda lango leo kwa asilimia 100 na kisha tukajaribu kutumia vyema fursa zetu, mbinu ambayo tunaitumia vyema sana na sidhani kama ni kandanda la kukera sana lakini kila mara sisi hufanya hivyo kuhakikisha lango letu halifungiki".

Wote wako nyuma ya Bayern Munich na pengo la pointi sita. Hamburg wanasalia katika nafasi ya 15. Msikilize kocha wao Markus Gisdol "Hatukufunga mabao na Schalke wakafunga. Vinginevyo niliona timu mbili zenye ubora sawa. Yule angefunga wa kwanza angeüpata ushindi na ukibaki nyuma badi hauwezi kushinda mechi kama hiyo".

Katika mechi nyingine ya jana, Werder Bremen hatimaye walipata ushindi wao wa kwanza wa msimu na wana kila sababu ya kumshukuru Max Kruse aliyewafungia mabao matatu katika ushindi wao wa nne bila. Borussia Dortmund sasa wako katika nafasi ya nne, baada ya kupea kipingo cha tatu mfululizo cha mbili moja dhidi ya VfB Stuttgart.

Bundesliga VfB Stuttgart v Borussia Dortmund
Mambo hayaendi vizuri katika kambi ya Dortmund Picha: Getty Images/Bongarts/M. Hangst

Bayern Munich siku ya Jumamosi walijiimarisha kileleni mwa ligi na pointi 29 baada ya kuwazidi nguvu mahasimu wao wa Bavaria Augsburg tatu bila. Ulikuwa ushindi wa 500 wa kocha Jupp Heynckes akiwa mchezaji au kocha. Ameshinda mechi nane mfululizo katika mashindano yote tangu aliporejea kama kocha. Matatizo ya FC Cologne yaliendelea baada ya kulazwa bao moja kwa sifuri na Mainz. Vijana hao bado wanaburura mkia na hawajashinda mechi yoyote mpaka sasa kitu kinachomkosesha usingizi kocha Peter Stoger "Mradi tu hakuna njia mbadala au jibu lakweli kwa hali hii, siwezi kusema kuwa naliacha jahazi hili linalozama. Sikwepi jukumu langu, siwezi tu kufanya kitu kama hicho, sikimbii mimi".

Borussia Moenchengladbach iliizaba Hertha Berlin mabao manne kwa mawili na kuruka hadi nafasi ya tatu kwenye Bundesliga. Christoph Kramer ni kiungo wa Gladbach na hakufurahishwa na mabao waliofungwa "Ndio kitu pekee tunapaswa kujilaumu kwa kiasi fulani, kwamba tuliongoza ugenini Berlin tatu bila. Ni wazi kuwa miguu yetu ilikuwa na uchovu kwa kiasi fulani na hatukuweza kumzuia mpinzani kwa urahisi lakini kitu kizuri ni kuwa hatukulegea baada ya kufungwa 3-2 kwa mawili. Tulizingatia mchezo wetu na mwishowe tukapata ushindi muhimu wa 4-2 ugenini".

Wolfsburg waliwapa kipigo Freiburg tatu moja na kumpa kocha Martin Schmidt  ushindi wake wa kwanza baada ya kuanza kazi kwa kupata sare kwenye mechi saba mfululizo. Hoffenheim ilitoka sare ya moja kwa moja na Eintrsacht Frankfurt.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP
Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman