1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

SHANGHAI: China yakanusha kupora raslimali ya Afrika

16 Mei 2007
https://p.dw.com/p/CC1a

Benki ya Maendeleo ya Afrika inayofanya mkutano wake wa mwaka mjini Shanghai,imeambiwa na waziri mkuu wa China Wen Jiabao kuwa China inataka kuwasaidia masikini barani Afrika kwa kuhimiza ukuaji wa kiuchumi.Wen alikanusha lawama kuwa China inataka kupora mafuta na madini ya bara Afrika na akaongezea kuwa serikali ya Beijing imetoa msaada wa Euro bilioni moja kupunguza madeni ya bara hilo.Amesema,China pia inayahimiza makampuni yake barani Afrika kushiriki katika miradi ya umma kama vile ujenzi wa barabara na matunzo ya afya.Kwa upande mwingine,Donald Kaberuka anaeongoza Benki ya Maendeleo ya Afrika ya madola 50 amesema,mkutano wa mjini Shanghai umetoa fursa kwa Afrika kujifunza kutokana na uzoefu wa Asia,kujitoa kwenye hali ya kutegemea misaada na kujiokoa kutoka mizozo ya fedha. Amesema,uchumi wa bara Afrika bado ni mchanga lakini kwa wastani,unakua kwa asilimia 5.5 kila mwaka.