Sherehe za kuadhimisha miaka 60 tangu kuundwa kwa Jamhuri ya watu wa China
1 Oktoba 2009Salamu hizi za hamjambo, marafiki na endeleeni na kazi kwa bidii, masahibu, kutoka kwa Rais Hu Jintao, aliyekuwa amebebwa katika gari lililokuwa wazi, ndizo zilifungua pazia la sherehe za kuadhimisha miaka 60 tangu kuundwa kwa Jamhuri ya watu ya China.
Gwaride kubwa kabisa la kijeshi na vifaa vya kijeshi, ikiwemo, ndege za kivita, vifaru vya kisasa na mitambo ya Satelite ilikuwa wazi kwa kila mmoja kujionea katika sherehe hizi- bila shaka China ilikuwa inataka kutuma ujumbe- tuko imara kijeshi na tunaendelea kuchukuwa nafasi ya ushawishi katika jukwaa la kimataifa.
Raia wa kawaida pia hawakuachwa nyuma katika shamra shamra hizi- zaidi ya laki moja watu waliungana na wanajeshi katika maonyesho yaliyokuwa na ujumbe aina tatu- mafanikio, itikadi pamoja na mtazamo wa baadaye wa Jamhuri ya China.
Rais Hu Jintao, baadaye alikamilisha sherehe za leo , kwa hotuba iliyoonyesha jinsi China ilivyopiga hatua kubwa hasa katika sekta ya uchumi. Hu aliwahakikishia raia wa China kwamba, chama tawala cha Kikomunisti kitaendeleza uchumi wa nchi hiyo, katika misingi ya uhusiano wa jamii zote kulingana na maadili ya Wachina pamoja na kuhubiri, umoja, utangamano na taifa imara.
Rais Hu Jintao pia alimlimbikizia sifa, Mao Zedong, aliyetangaza kuundwa kwa Jamhuri ya China miaka 60 iliyopita. Pamoja na Ze Dong, Hu pia aliwakumbuka viongozi wengine wa chama hicho, Deng Xiapoing na Jiang Zemin akisema wamechangia katika ufanisi wa chama cha kikomunisti na China kwa jumla.
Sherehe za leo zilifanyika katika uwanja wa Tianamen Square, eneo lililokuwa uwanja wa mauti, mwaka wa 89, baada ya mamia ya waandamanaji kuuawa katika maandamano ya kutaka demokrasia nchini China.
Hong Kong ambayo ipo chini ya utawala wa China tangu mwaka wa 97, pia iliadhimisha sherehe hizi, huku kiongozi wa Hong Kong akisema China imekuwa injini ya kusukuma gurudumu la uchumi duniani.
Mwandishi: Munira Muhammad/DPAE
Mhariri: Kitojo.