Shinikizo lazidi makali dhidi ya serikali ya Syria
1 Agosti 2011"Wakati umewadia kwa baraza la usalama la Umoja wa mataifa kuchukua msimamo bayana kutokana na umuhimu wa kukomeshwa matumishi ya nguvu" amesema bibi Catherine Ashton katika taarifa yake.
Baraza la Usalama la Umoja wa mataifa limepanga kukutana baadae hii leo kwa kikao cha adharura.
Laana zimehanikiza tangu jana kutoka kila pembe ya dunia baada ya jeshi la Syria kuuvamia mji wa Hama na kuwauwa mamia ya watu.Umoja wa Ulaya unazungumzia juu ya mauwaji.
Rais Barack Obama amesema "ameshutushwa" na jinsi hali namna ilivyo na kuahidi Washington itafzidisha juhudi kutaka serikali ya Damaskus izidi kutengwa.Italy na Ujerumani zimetoa mwito baraza la usalama likutane haraka huku waziri wa mambo ya nchi za nje wa Uengereza William Hague akisema
"Tunataka shinikizo la kimataifa lizidi dhidi ya Syria,ikiwa ni shinikizo kutoka nchi za magharibi,nchi za kiarabu na Uturuki pia."
Nae waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ubeligiji Steven Vanackere amesema kwa upande wake anaunga mkono msimamo wa Ujerumani na Ufaransa kutaka mjadala wa kina ufanyike katika baraza la usalama,ili kutoa ishara kwa utawala wa Syria ukomeshe haraka matumizi ya nguvu.
Kwa upande mwengine muakilishi mkuu wa siasa ya nje ya Umoja wa Ulaya amethibitisha uamuzi wa Umoja wa ulaya wa kuwawekeya vikwazo maafisa wengine watano walio karibu zaidi na rais Bachar al Assad.
"Leo jumatatu,Umoja wa Ulaya umeamua kuwachukulia hatua ziada,ikiwa ni pamoja na kuzuwiliwa mali zao na kupigwa marufuku wasiingie katika nchi za Umoja wa Ulaya watu watano wanaohusika na visa vya ukandamizaji nchini Syria-amesema muakilishi mkuu huyo wa siasa ya nje ya Umoja wa ulaya.Majina ya wahusika yatatangazwa gazeti rasmi la Umoja wa ulaya hapo kesho.
"Kwa wakati wote ambapo serikali ya Syria itaendelea kutumia nguvu dhidi ya wanaharakati wanaodai mageuzi,Umoja wa Ulaya utaendeleya na sera yake ya sasa ikiwa ni pamoja na kuwawekea vikwazo wale wote wanaohusika na kuwatumilia nguvu waandamanaji,amemaliza kusema bibi Catherine Ashton.
Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/afp,reuters
Mhariri: Abdul-Rahman,Mohammed