1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

SOFIA: Libya yaikosoa Bulgaria kwa kuwasamehe wafungwa

26 Julai 2007
https://p.dw.com/p/CBf3

Libya leo imeishutumu Bulgaria kwa kuvunja makubaliano yaliyofikiwa baina ya nchi hizo mbili kwa kuwasamehe wataalamu sita wa afya.

Wataalamu hao walihukumiwa na mahakama ya Libya kifungo cha maisha gerezani kwa kuwaambukiza watoto zaidi ya 400 virusi vya ukimwi katika hospitali ya Bengazi nchini Libya.

Wataalam hao walirejeshwa Bulgaria mapema wiki hii baada ya makubaliano kufikiwa baina ya Libya na Umoja wa Ulaya.

Msemaji wa wizara ya mashauri ya kigeni wa Bulgaria amesema uamuzi wa rais wa Bulgaria kuwasamehe wauguzi watano wa Bulgaria na daktari mmoja mpalestina ni kwa mujibu wa sheria za nchi hiyo.

Aidha amesema Bulgaria inaheshimu sheria za Libya na taasisi zake na ameitaka Libya ichukue hatua kama hiyo.

Tangazo rasmi la Libya kuilaumu Bulgaria limetolewa siku moja baada ya familia za watoto walioambukizwa ukimwi kuilaani vikali Bulgaria na kuitaka serikali mjini Tripoli ikate uhusiano wake wa kidiplomasia na nchi hiyo.