1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Soka:MANU yashindwa kupita darajani

2 Machi 2011

Chelsea jana ilipambana kiume kuweza kusawazisha bao na hatimaye kufunga la ushindi dhidi ya Manchester United katika mechi ya ligi kuu ya nchi hiyo Premier League.

https://p.dw.com/p/10Rpz
Mshambuliaji wa Manchester United Wayne Rooney baada ya kutolewa na ChelseaPicha: AP

Katika pambano hilo lililofanyika kwenye uwanja wa Chelsea Stamford Bridge, United walikuwa wa kwanza kufunga bao kupitia kwa mshambuliaji wake Wyne Rooney kwenye dakika ya 29.

Lakini beki aliyesajiliwa hivi karibuni kutoka Ureno mbrazil David Luiz aliisawazishia Chelsea bao hilo dakika nane tokea kuanza kwa kipindi cha pili kwa mkwaju mkali akiwa ndani ya 18.

Chelsea walionesha uhai, walifanya mashambulizi kadhaa  ambapo katika dakika ya 79 Yuri Zhirkov aliangushwa ndani ya eneo la hatari, ambapo mwamuzi hakuwa na hiyana ila kuipa Chelsea penalti iliyotumbikizwa kimiani na Frank Lampard.

Ushindi huo wa Chelsea umeifanya kuendeleza rekodi yake ya kutofungwa na Manchester United katika uwanja wake wa Stamford Bridge tokea mwaka 2002.

Hata hivyo pamoja na kufungwa, Manchester United bado inaongoza ligi hiyo ikiwa na pointi 60, pointi 12 zaidi ya Chelsea wanaotetea ubingwa wao.Chelsea wana pointi 48.

Nafasi ya pili inashikiliwa na Arsenal wenye pointi 56, lakini wakiwa na mchezo mmoja pungufu, huku Manchester City wakikamata nafasi ya tatu kutokana na pointi 50 ilizotia kibindoni.

Mwandishi:Aboubakary Liongo/Reuters

Mhariri:Mohamed Abdulrahman