1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Sudan yatuhumiwa kutumia silaha za sumu

Bruce Amani
29 Septemba 2016

Serikali ya Sudan imefanya mashambulizi 30 yanayoshukiwa kuwa ya silaha za sumu katika eneo la Jebel Marra jimboni Darfur tangu Januari mwaka huu ikitumia kile watalaamu wamesema ni kemikali ya kusababisha malengelenge

https://p.dw.com/p/2QipF
Anja Niedrighaus Preis 2016, Foto von Adriane Ohanesian
Picha: A. Ohanesian

Amnesty International imekadiria kuwa karibu watu 250 huenda walifariki kutokana na silaha za kemikali. Shambulizi la karibuni kabisa lilifanyika Septemba 9 na Amnesty imesema uchunguzi wake ulizingatia picha za satelaiti, mahojiano na zaidi ya watu 200 na watalaamu kuchunguza picha zilizoonyesha majeraha.

Mkurugenzi wa utafiti wa migogoro wa shirika la Amnesty International Tirana Hassan amesema matumizi ya silaha za sumu ni uhalifu wa kivita ""wakati wa mashambulizi haya, mamia ya raia walipigwa risasi, maelfu walipoteza makaazi, na moja ya mambo yanayokasirisha zaidi katika mgogoro wa Darfur ni kuwa tumepata ushahidi wa kuaminika kuwa serikali ya Sudan imekuwa ikitumia silaha za sumu dhidi ya raia"

Sudan Darfur Konflikt Soldaten
Wapiganaji wa kikosi cha Sudanese Rapid Support Forces katika jimbo la DarfurPicha: Getty Images/AFP/A. Shazly

Balozi wa Sudan katika Umoja wa Mataifa Omer Dahab Fadl Mohamed amesema katika taarifa kuwa ripoti hiyo ya Amnesty "haina msingi wowote kabisa” na kuwa Sudan haimiliki aina yoyote ya silaha za sumu. Amnesty imesema iliwakabidhi matokeo ya uchunguzi wake kwa watalaamu huru wa silaha za sumu. "tuliwapa watalaamu huru wawili ushahidi wote tuliokusanya. Waliuangalia na wakasema kuna ushahidi wa kuaminika kuwa kumekuwa na matumizi ya aina Fulani ya kemikali na hasa, kuna uwezekano mkubwa wa matumizi ya kemikali ya kusababisha malengelenge"

Sudan ilijiunga katika Makubaliano ya Silaha za Sumu mwaka wa 1999 ambapo wanachama hukubali kutotumia silaha za sumu.

Jeshi la kulinda amani la Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa, linalofahamika kama UNAMID, limekuwa Darfur tangu mwaka wa 2007. Usalama bado ni tete jimboni humo, ambapo makabila yasiyo ya waarabu yanapigana na serikali ya Khartoum inayoongozwa na waarabu, na serikali inajitahidi kuyadhibiti maeneo ya mashambani. Karibu watu 300,000 wameuawa Darfur tangu mzozo huo ulianza 2003, kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, wakati watu milioni 4.4 wanahitaji msaada na wengine milioni 2.5 wamepoteza makaazi.

Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ilitoa waranti za kukakamatwa Rais wa Sudan Omar Hassan al-Bashir mwaka wa 2009 na 2010 kwa tuhuma za uhalifu wa kivita na mauaji ya halaiki kutokana na operesheni yake ya kuangamiza uasi wa Darfur.

Mwandishi: Bruce Amani/reuters
Mhariri:Iddi Ssessanga