1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

TAIPEI: Maandamano yafanyika kuunga mkono uanachama wa Taiwan katika Umoja wa Mataifa

16 Septemba 2007
https://p.dw.com/p/CBPT

Maelfu ya raia nchini Taiwan wameandamana katika miji miwili mikubwa ya nchi hiyo kuuambia ulimwengu kwamba kisiwa hicho kina haki kujiunga na Umoja wa Mataifa.

Wakiongozwa na rais wa Taiwan, Chen Shui-bian, wafuasi wa chama tawala cha Democratic Progess Party, DPP, waliandamana katika barabara za mji mkuu Taipei wakitaka ulimwengu ukiunge mkono kisiwa hicho kutaka kuwa mwanachama wa Umoja wa Mataifa.

Chama cha DPP, kinataka kufanyike kura ya maoni kisiwani humo kiweza kuwasilisha ombi kwa Umoja wa Mataifa kutumia jina la Taiwan, jambo ambalo linapingwa vikali na China na Marekani.

Katika maandamano mengine nchini Taiwan chama cha upinzani cha KMT kimefanya maandamano kupinga kura hiyo ya maoni.

Aliyekuwa balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, John Bolton, anaunga mkono Taiwan kuwa mwanachama wa umoja huo.

´Ama kweli kuna watu wengi katika wizara ya mambo ya ndani ya Marekani ambao wanaonekana wanataka kujua mengi kuhusu utawala wa kiimla wa Korea Kaskazini badala ya kuitambua demokrasia nchini Taiwan.´

Chama tawala cha DPP kimesema watu takriban nusu milioni walihudhuria mkutano wa hadhara uliofanyika katika mji wa kusini wa Kaohsiung, lakini polisi imesema ni watu laki moja na nusu walioandamana mjini humo.