1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tamko la serikali ya Ujerumani juu ya Afghanistan.

Abdu Said Mtullya22 Aprili 2010

Kwa mara nyingine Kansela Merkel atetea jukumu la Afghanistan.

https://p.dw.com/p/N3t8
Kansela Angela Merkel wa Ujerumani.Picha: AP


Kansela wa Ujerumani Angela Merkel kwa mara nyingine ametetea jukumu la Afghanistan linalotekelezwa na wanajeshi wa nchi yake. Kansela Merkel amesema hayo leo kwenye bunge la Ujerumani.

Akiwahutubia wabunge kufafanua msimamo wa serikali ya Ujerumani juu ya jukumu la Afghanistan, Kansela Merkel amesema usalama wa Ujerumani unategemea ushindi dhidi ya wapinzani wa kitaliban nchini Afghanistan.

Katika tamko hilo kiongozi huyo wa Ujerumani pia aliwaenzi askari saba wa Ujerumani waliouawa Afghanistan mnamo wiki za hivi karibuni.Merkel amesema jukumu la Afghanistan linawafiki na sheria za kimataifa na katiba ya Ujerumani.

Bibi Merkel ametahadharisha kwamba panaweza kutokea maafa makubwa zaidi ya yale ya mashambulio ya tarehe 11 mwezi septemba nchini Marekani ikiwa majeshi ya kimataifa yataondoka mapema Afghanistan.Ameeleza kuwa hatari kubwa inatokana na uwezekano wa magaidi kupata silaha za nyuklia.

Akitetea uamuzi wa kutekeleza jukumu la Afghanistan Merkel amesema jumuiya ya kimataifa iliingia Afghanistan pamoja na kwa hiyo itaondoka pamoja.Hata hivyo amesema itakuwa hatari kuondoka Afghanistan bila ya mpango maalumu.

Lakini mwenyekiti wa chama cha mrengo wa shoto Gregor Gysi ametaka kuondolewa haraka kwa wanajeshi wa Ujerumani kutoka Afghanistan.Hata hivyo amesema haitakuwa sawa kuondoka bila ya mpango.

Mwandishi/ Mtullya Abdu DPAE/ZA

Mpitiaji:Abdul-Rahman