1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

TEHRAN: Iran yataka raia wake waachiliwe

15 Januari 2007
https://p.dw.com/p/CCaQ

Iran inataka raia wake watano wanaozuiliwa na Marekani nchini Irak waachiliwe huru mara moja. Wairan hao walitiwa mbaroni mnamo Alhamisi wiki iliyopita mjini Arbil kaskazini mwa Irak na wanashtakiwa kwa kuwa na mafungamano na kundi la mapinduzi la Iran linalowapa silaha wapiganaji wa Irak.

Msemaji wa wizara ya mambo ya kigeni wa Iran amesema watuhumiwa wote watano ni wanadiplomasia. Hata hivyo msemaji wa Marekani Stephen Hadley amesema watu hao wanafanya vitendo visivyokubalika nchini Irak.

´Alichokiweka wazi rais ni kwamba hivi vitendo vinavyoendelea nchini Irak ambavyo havikubaliki vinayahatarisha maisha ya watu wetu. Na amesema wazi kwamba tutachukua hatua.´

Wakati huo huo, rais wa Iran Mahmoud Ahmadinejad amefanya mazungumzo na rais wa Nicaragua, Daniel Ortega. Ahmadinejad yumo katika ziara ya mataifa ya Amerika Kusini ambayo hayaipendelei Marekani, katika juhudi za kutafuta uungwaji mkono kuhusiana na mpango wake wa nyuklia huku nchi yake ikikabiliwa na shinikizo la mataia ya magharibi.